WAZIRI wa Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo innocent Bashungwa amewataka watanzania kwa pamoja kuinga mkono klabu ya Simba kwenye mchezo wa marudiano wa robo fainali dhidi ya Kaizer Chiefs kwa kuwa timu inaposhinda na kuiwakilisha nchi inakuwa ni timu ya Taifa. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mchezo huo wa marudiano utachezwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam Jumamosi ya tarehe 22 Mei, 2021 majira ya saa 10 jioni, huku kwenye mchezo wa awali uliochezwa Afrika Kusini Simba ilipoteza kwa mabao 4-0.
Waziri Bashungwa ameyasema hayo leo tarehe 19 Mei, 2021 Bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Makete (Cccm) Festo Sanga ambaye alitaka kujua serikali inamkakati gani kuhakikisha Simba inaibuka na matokeo kwenye mchezo huo na mashabiki wanajaa Uwanjani.
Katika majibu yake Bashungwa alisema kuwa serikali itashirikiana kwa karibu na klabu ya Simba ili kufanikisha kufanya vizuri kwenye mchezo mara ambao wanahitaji ushindi wa hali na mali na kuwataka watanzania kuwaunga mkono.
“Timu inaposhinda na kuiwakilisha nchi yetu inakuwa ni timu ya Taifa, nitoe wito kwa watanzania kuiunga mkono Simba ili ifanye vizuri kwenye mchezo huo wa tarehe 22 Mei, 2021 dhidi ya Kaizer Chiefs na sisi serikali tutashirikiana nao kwa karibu.” Alisema Bashungwa
Kwenye mchezo huo Simba anahitaji ushindi wa kuanzia mabao 5 na kuendelea ili iweze kufuzu kwenye hatua ya nusu fainali bila ya nyavu zao kutikiswa.
Tayari kikosi hiko kimeshaingia kambini siku ya jana tayari kwa ajili ya maandalizi ya mchezo huo mara baada ya kurejea siku ya Jumatatu kutoka Afrika Kusini na kocha wa kikosi hiko Didier Gomes alinukuliwa akisema kuwa “Tutahitaji kuwa bora ili tupate matokeo kwenye mchezo wa marudiano”
Leave a comment