WAZIRI wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Innocent Bashungwa amekitaka Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwekeza kwenye michezo kwa kuwa inamiliki asilimia kubwa ya viwanja hapa nchi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Bashungwa amesema hayo hii leo tarehe 25 Februari 2021, katika muendelezo wa ziara ya Rais Magufuli jijini Dar es Salaam kwenye viwanja wa Mnazi Mmoja alipokuwa akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa soko la Kisutu.
Wakati akitoa salamu zake Bashungwa alisema pamoja CCM kuwekeza kwenye tasnia ya habari lakini pia chama hiko kina nafasi ya kuwekeza kwenye michezo kwa kukarabati viwanja vyake ili viweze kusaidia hapo mbeleni.
“Najua chama changu CCM, Mmewekeza kwenye tasnia ya habari, lakini mnayo nafasi ya kuwekeza kwenye michezo kwa kuwa CCM inamiliki viwanja vingi,” alisema Bashungwa.
Aidha Waziri huyo alichukua fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji wenye nia ya kuwekeza kwenye viwanja hivyo ambavyo kwa asilimia kubwa vinatumika kwenye michezo ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
“Nitumie nafasi hii kukaribisha wawekezaji wagonge hodi kwenye wizara yetu ya michezo na sisi tunawapeleka kwenye chama chetu ili viwanja hivi viweze kusaidia kwenye michezo mbalimbali,” aliongezea waziri huyo.
Mpaka sasa kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara viwanja saba vinavyomilikiwa na CCM, vimetumika na timu mbalimbali katika michezo yao ya nyumbani.
Viwanja hivyo ni Kaitaba mkoani Kagera unaotumiwa na Kagera Sugar, Uwanja wa Jamhuri uliopo Dodoma unaotumiwa na klabu za JKT Tanzania na Dodoma Jiji, Jamhuri mkoani Morogoro unaotumiwa na Mtibwa Sugar kwenye michezo yake ya nyumbani inapocheza na klabu za Simba na Yanga.
Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya unaotumia na klabu ya Mbeya City pamoja na Ihefu FC kwa baadhi ya michezo, Kambarage Shinyanga unaotumiwa na Mwadui FC, CCM Mkwakwani jijini Tanga unaotumiwa na Coastal Union, Uwanja wa Karume uliopo Mara unaotumiwa na klabu ya Mwadui FC pamoja na dimba la Nelson Mandela mkoani Shinyanga.
Viwanja hivi vinatumika mara kwa mara kutokana na asilimia kubwa ya timu zinazoshiriki Ligi Kuu na Ligi daraja la kwanza kutokuwa na viwanja vyake binafsi kama ilivyo kwa klabu zingine.
Leave a comment