WAZIRI wa Kilimo nchini Tanzania, Hussein Bashe amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali wa Benki ya NMB akiwemo Mkuu wa Idara ya Kilimo na Biashara, Isaac Masusu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Mazungumzo hayo mafupi, yalifanyika jana Jumanne tarehe 17 Mei 2022 katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma, mara baada ya Waziri Bashe kumaliza kuwasilisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka 2022/23.
Katika mazungumzo hayo, Masusu aliongozana na Mkuu wa Idara ya Ubunifu, Josina Njambi na maofisa mbalimbali wa NMB ambao kwa pamoja walipata fursa ya kupiga picha ya pamoja.
Katika picha hiyo akikuwemo, Naibu waziri wa wizara hiyo, Anthony Mavunde na Katibu Mkuu wa wizara hiyo Andrew Masawe.
Akiwasilisha bajeti yake, Waziri Bashe alisema, imeongezeka kwa mafungu yote matatu kutoka Sh.294.16 bilioni hadi Sh.751.12 bilioni sawa na ongezeko la asilimia 155.34.
Alisema sehemu kubwa ya fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, miundombinu ya uhifadhi wa mazao, kuimarisha upatikanaji wa masoko ya mazao, kuimarisha utafiti wa kilimo, uzalishaji wa mbegu na utoaji wa ruzuku.
Aidha, Waziri Bashe alizishukuru taasisi mbalimbali za kibenki ikiwemo NMB kwa kushiriki kwenye sekta ya kilimo kwa kutoa mikopo pamoja na kupunguza viwango vya riba.
Alisema hatua hiyo imepelekea benki ya NMB kutenga Sh.100 bilioni kwa ajili ya kukopesha wajasiriamali katika sekta ya kilimo kupitia matawi yake 225 nchi nzima.
Waziri Bashe alisema, mikakati mingine ni mauzo ya mazao kupitia vyama vya ushirika yataimarishwa kwa itaendelea kuimarisha kujenga ghala chini ya mpango utakaohusisha Tume ya Maendeleo ya Ushirika na benki ya NMB.
Leave a comment