WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso amewataka wahandisi na wakandarasi kujiandaa na mabadiliko yatakayofanyika yenye lengo la kuboresha ufanisi. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Aweso ametoa kauli hiyo leo Ijumaa, tarehe 23 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma, ikiwa ni siku moja tangu Rais Samia Suluhu Hassan, alipolihutubia Bunge na kumtaka Aweso, kusimamia sekta ya maji.
Rais Samia amesema, kutafanyika mabadiliko makubwa kwa wahandisi ili kuongeza ubora wa usimamizi wa maji lengo ni kihakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi huku akimwonya Waziri Aweso kwamba, akishindwa kusimamia atapaswa kuondoka.
Leo Ijumaa bungeni, Aweso akimsaidia naibu waziri wa wizara yake, Maryprisca Mahundi kujibu maswali ya nyongeza ya wabunge, yaliyohusu upatikanaji wa maji amesema “wahandisi wa maji na wakandarasi wakae sawa. Tumeanza kufanyia kazi maagizo ya mheshimiwa Rais.”
Katika swali la msingi, Mbunge wa Manyoni Magharibi (CCM), Dk. Pius Chaya amehoji “Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa maji wa Kintinku-Lusilile ili Wananchi wa Vijiji 11 vya kata ya Chikuyu, Makutupora, Maweni na Kintinku waanze kupata maji safi na salama.”

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri, Maryprica amesema, mradi wa maji Kintinku/Lusilile ni mradi mkubwa ambao unatekelezwa kwa awamu nne hadi Machi 2021, utekelezaji awamu ya kwanza ulifikia asilimia 90 kwa gharama ya Sh.2.085 Bilioni.
“Kazi zilizofanyika ni pamoja na ufungaji wa mitambo ya kusukuma maji, ujenzi wa nyumba za mtambo wa kusukuma maji, tanki la kukusanya maji la lita laki tatu na ujenzi wa tanki la kuhifadhi na kusambaza maji la lita milioni mbili na ulazaji wa bomba kuu umbali wa Kilometa 1.2,” amesema Maryprisca
“Pia, Vijiji vitatu vya Chikuyu, Mwiboo na Mbwasa, vinatarajia kuanza kupata huduma ya maji Juni,” amesema.
Aidha Serikali kupitia RUWASA imepanga kukamilisha usambazaji wa maji katika Vijiji vyote 11 katika mwaka wa fedha 2021/22 na utahudumia wakazi zaidi ya 55,000.
Leave a comment