NAIBU Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Juma Aweso amemsimamisha kazi Meneja wa Mamlaka ya Maji Misungwi, Charles Kampuni pamoja na kuvunja bodi ya maji ya mamlaka hiyo kwa kuchangisha wananchi pesa bila utaratibu. Anaripoti Moses Mseti, Misungwi … (endelea).
Meneja wa Mamlaka hiyo pamoja na bodi hiyo wanatuhumiwa kuchangisha fedha kwa wananchi kiasi cha Tsh. 45 milioni bila kuwashirikisha wananchi kitendo ambacho ni kinyume na utaratibu.
Aweso amechukua maamuzi hayo baada ya kupokea kero kutoka kwa wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika jana mjini Misungwi na kubaini uwepo wa tuhuma hizo.
“Mmewachangisha pesa bila kuwashirikisha na nyie mnasema mlisahau, mnasahau kufanya mikutano alafu mnakurupuka kuchukua fedha zao na kwa mambo haya mliyoyatafanya tunakusimamisha na tutakutafutia kazi ya kufanya.
“Mimi sina maneno ya kumung’unya na lengo letu ni wananchi wa Misungwi kupata maji, kuanza sasa tumevunja rasmi bodi ya Misungwi kuanzia leo na hizo fedha za wananchi lazima tufahamu zimeenda wapi,” alisema Aweso.
Kutokana na fedha hizo kutokujilikana zipo wapi, Naibu waziri Aweso alimwagiza Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Antony Sanga, kumpeleka mkaguzi wa ndani wa wizara hiyo kukagua fedha zilivyotumika na zimefanya kazi gani.
Alisema kuwa baada ya mkaguzi huyo wa wizara kufanya ukaguzi, itasaidia kubaini watu waliopiga fedha hizo za wananchi hatua itakayosaidia kila mmoja kubeba msalaba wake.
Katika hatua nyingine, Waziri Aweso alitembelea mradi mkubwa wa maji wa Magu wenye gharama ya Tsh. 16.9 bilioni ambao tayari umekamilika na umeanza kutoa huduma kwa wananchi wa mji wa Magu.
Mhandisi Sanga, alisema mradi huo umekamilika kwa asilimia 99 na kwamba vitu vidogo vidogo vilivyokuwa vimebaki tayari vimefanyiwa kazi.
Leave a comment