WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi nchini Tanzania, Dk. Leonard Chamuriho amewataka mafundi sanifu 15,260 ambao wamehitimu katika vyuo mbalimbali nchini kujisajili kwa Bodi ya Usajili Wahandisi (ERB), ili waweze kutambulika na kutumiwa katika kutekeleza miradi ya kimkakati nchini. Anaripoti Seleman Msuya, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Chamuriho ametoa kauli hiyo leo Ijumaa, tarehe 23 Julai 2021, wakati akifungua Kongamano la Tatu la Mafundi Sanifu lililofanyika jijini Dar es Salaam ambapo zaidi ya wanataaluma 500 wa kada hiyo wameshiriki.
Amesema kongamano hilo ambalo lilibeba kauli mbiu ‘Mchango wa mafundi sanifu katika maendeleo ya teknolojia na ubunifu’ ni imani yake kuwa washiriki watatoka na mwelekeo wa pamoja katika kutumia taaluma zao kuchochea maendeleo ya viwanda.
Waziri huyo amesema, takwimu kwmaba mafundi sanifu walisajiliwa ni 1,707 hazifurahishi hivyo kuwataka waliobakia kujisajili ERB kwa kuwa kutokufanya hivyo ni kinyume na sheria za nchi.
Amesema ni wazi kuwa uwiano kati ya wahandisi, mafundi sanifu na mafundi stadi haulingani lakini uchache wa mafundi sanifu waliojisajili ERB haoneshi picha nzuri katika eneo hilo.
“Taarifa nilizonazo ni kwamba kwa miaka 10 iliyopita mafundi sanifu waliohitimu katika vyuo vyetu ni 15,260 ila waliosajiliwa ERB ni 1,707 hii sio sawa. Natoa wito kwa mafundi sanifu wote ambao hawajajisajili wajisajili kwani ni kosa kisheria kufanya kazi bila kujisajili.”
“Viwango vya uwiano wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), unataka mhandisi mmoja afanye kazi na mafundi sanifu watano na mafundi stadi 25 jambo ambalo hapa nchini kwa sasa limeshindikana,” amesema Dk. Chamuriho
Amesema, mafundi sanifu ni kada muhimu katika maendeleo ya nchi hasa katika ujenzi wa viwanda na miradi mbalimbali.
Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya ERB, Profesa Ninatubu Lema amesema kada ya mafundi sanifu ni muhimu katika kufanya mapinduzi ya viwanda na uchumi hivyo kuiomba Serikali kuwekeza katika eneo hilo.
Mhandisi Lema amesema ERB itahakikisha inashirikiana na Serikali kuwa kada ya mafundi sanifu inapewa nafasi kwenye miradi mbalimbali ya kimkakati ili washiriki kuchochea maendeleo.
Kwa upande wake, Msajili wa ERB, Mhandisi Patrick Barozi, amesema bodi hiyo hadi sasa imesajili wahandisi 31,729, mafundi sanifu 1,707 na kampuni ya ushauri 382.
Barozi amesema kongamano hili linalenga kutambua umuhimu wa kada hiyo kwa maendeleo ya taifa, kuonesha umma namna wanaweza kuchochea maendeleo, kuwezesha umma kutambua mchango wa kada hiyo na kuwatambua mafundi sanifu walitoa mchango kwenye maendeleo ya nchi.
“Pia tunatumia kongamano hili kuwawezesha wajiri na watumiaji wa huduma kutambua uwezo wao, kuwatia moyo wanafunzi wanaosoma masomo ya ufundi sanifu na kuwaunganisha mafundi sanifu pamoja,” amesema.
Leave a comment