WILLIAM Ole Nasha, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, amewataka wakuu wa shule nchini kushawishi wanafunzi kuchangamkia fursa za mashindano ya uandishi wa Insha za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo 11 Desemba 2019, jijini Dodoma hafla ya kutunuku vyeti kwa washindi wa kitaifa wa Shindano la Uandishi wa Insha za SADEC na EAC.
Amesema, uandishi wa Insha za SADEC na EAC utaweza kuwasaidia na kuwaongozea uwezo wanafunzi katika kukuza ujuzi wa lugha.
“Napenda kusisitiza kuwa, wakuu wote wa shule kuendelea kuwashawishi wanafunzi kuchangamkia fursa za mashindano kwani pamoja na kuwaongozea uwezo wao katika kukuza ujuzi wa lugha, uandishi wa insha unaongeza maarifa kwa ujumla,” amesema.
Naibu Waziri huyo aliwataka pia Wakuu hao kusimamia kwa umakini mchakato wa mashindano hayo ili kuhakikisha ushiriki wa wanafunzi wengi.
“Nawaagiza kila Mkuu wa shule kuteua mratibu atakayefanya kazi ya kusimamia wanafunzi ili wazingatie na kufuata taratibu zote za uandishi wa insha ili tuweze insha nzuri na kuziwasilisha katika mashindano ya kanda,”amesema.
Naye,Mratibu wa Shindano hilo,Sylvia Chinguwile alimtangaza, Vanessa Lema kutoka Shule ya Sekondari Longodo Mkoani Arusha ambaye yupo kidato cha nne kuwa mshindi wa shindano hilo.
Wengine walioshinda katika shindano hilo ni Thomas Kalisha mwanafunzi wa kidato cha tatu kutoka shule ya Kibasila ya Jijini Dar es salaam ambaye alishika nafasi ya pili,huku nafasi ya tatu ikishikwa na Monica Nyamhanga mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya Sekondari Heritage ya Mkoani Pwani.
Leave a comment