JUMLA ya kaya za wazee 10 za kata ya Ngerengere wilayani Morogoro mkoani hapa zimekabidhiwa kadi za mfuko wa Bima ya Afya ya Jamii (CHF) iliyoboreshwa bure ili ziweze kupata huduma ya matibabu na dawa kwa wepesi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Akipokea kadi hizo jana mmoja wa wazee hao Saidi Tanganyika (71), mkazi wa kijiji cha Ngerengere aliipongeza Serikali kupitia mradi wa Tuimarishe Afya (HPSS) unaofadhiliwa na Serikali ya Uswisi kwa kuwapatia kadi hizo kwa zinazotolewa kwa gharama kubwa ambayo kwao ingekuwa shida kuipata.
Tanganyika, alisema wamepokea kadi hizo kama mkombozi wa maisha yao, kwani hapo awali walipata matibabu kwa shida kutokana na kutokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu wala kupata kadi hizo.
Naye Haruna Mohamed (80) mkazi wa Ngerengere akitoa shukrani zake kwa CHF na HPSS alisema kwa sasa watapata huduma ya matibabu na dawa kwa urahisi kutokana na kadi za sasa kuboreshwa tofauti na za awali ambazo ilikuwa lazima utibiwe katika eneo ulilopewa, ambapo alisema, licha ya kuwa na kadi haikuwa rahisi kupata dawa wakati wa matibabu.
“zamani ulikuwa unatibiwa pale tu ulipopewa kadi, lakini dawa ukanunue, lakini sasa kadi ni tofauti, serikali inatujali tunapata dawa, tunaomba huu mradi uwe endelevu” alisema Mohamed.
Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Kebwe Steven Kebwe alisema, aliwaasa wananchi hasa wakulima kukitumia vyema kipindi cha mavuno katika kupata kadi za CHF kwani ndio mkombozi katika maisha yao.
“hiki ni kipindi kizuri kuongea na wananchi juu ya mfuko wa CHF ulioboreshwa kwani ni kipindi cha mavuno na wananchi wanafedha na wanaweza kujiunga” alisema Kebwe.
Aidha aliwatoa hofu wananchi wanaodhani dawa bado hakuna hospitali kwa kusema, kwa sasa kikwazo cha kukosa dawa kwa wale wenye kadi hakipo ambapo mgonjwa anaweza akatibiwa na kupatiwa dawa kwa zaidi ya asilimia 95.
Akizungumzia Mradi huo, Meneja mradi wa Kuimarisha Afya (HPSS) Dk. Haruni Machibya, aliitaka jamii kuhamasiaka na kujiunga kwenye CHF kwani alisema, ugonjwa huwa haupigi hodi ili ukusubiri ujiandae.
Alisema nia ya CHF ni kuboresha mapato katika halmashauri kwa kuandikisha wanachama wengi zaidi ili vituo vipate fedha kwa ajili ya kununua dawa, vitendanishi na vifaa tiba, na hivyo kupelekea kiwango cha mteja kupata kadi kupanda kutoka sh. 10,000 mpaka 30,000.
Alisema, mradi huo una hafua mbili katika mkoa wa Morogoro tangu mwaka 2016, ambao ni Huduma ya afya ya jamii pamoja na uboreshaji wa upatikanaji wa dawa katika vituo ya afya vya serikali.
Hivyo aliongeza kuwa uzinduzi huo umefanyika katika kata ya Ngerengere kutokana na halmashauri hiyo kufanya vibaya kimkoa na kushika asilimia mbili ikilinganishwa na hamashauri nyingine kama Ifakara na Malinyi.
Leave a comment