BARAZA la Wazee la Mkoa wa Dar es Salaam, limemuomba Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, aongeze juhudi katika uimarishwaji misingi ya utawala bora. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es salaam..(endelea).
Wito huo umetolewa leo Ijumaa, tarehe 7 Mei 2021 na Salum Matimbwa, Mwenyekiti Baraza la Wazee Mkoa wa Dar es Salaam, katika Mkutano wa Rais Samia na Wazee wa mkoa huo, unaofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City.
“Kuhusu utawala bora, tunakupongeza kwa jinsi ambavyo wewe na serikali yako mnavyosimamia na kutekeleza masulaa mbalimbali ya utawala bora katika nchi yetu, ombi letu tunaomba juhudi hizi ziendelee katika kushughulikia kero za wananchi pamoja na malalamiko yao,” amesema Mzee Matimbwa.
Wakati huo huo, Mzee Matimbwa ameiomba Serikali ya Rais Samia, iwashirikishe wananchi katika masuala mbalimbali ikiwemo kwenye utafutaji suluhu za changamoto zao.
“Sambamba na hilo, tunaomba vyombo vya ulinzi na usalama kufanya kazi kwa kufuata sheria, kanuni na miongozi na pale inapobidi wananchi washirikishwe ipasavyo kuondoa matatizo madogo madogo. Hili kama mnavyo lisimamia vizuri likiendelezwa ustawi wa utawala bora na usalama utaendelea katika nchi yetu,” amesema Mzee Matimbwa.
Leave a comment