HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imekamilisha utambuzi wa wazee 19, 543 katika kata zote 41 za jiji hilo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hatua hiyo ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Wazee ya Mwaka 2003, inayolenga kuwaenzi kwa mchango wao katika Taifa kwenye nyanja mbalimbali ikiweno uchumi, siasa, kijamii na kiutamaduni.
Halmashuri hiyo pia tayari imewapatia vitambulisho wazee 10,290 ambavyo vitawatambulisha katika maeneo mbalimbali ya huduma ikiwemo kwenye vituo vya afya, huku wengine 2,686 vitambulisho vyao vikiwa katika maandalizi.
Rebeka Ndaki, Ofisa Ustawi wa Jamii alitoa taarifa hiyo ya halmashauri ya jiji hilo kwenye mkutano wa uzinduzi wa baraza hilo leo tarehe 8 Julai 2019, katika ukumbi Halmashauri ya Jiji, mbele ya Patrobas Katambi, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma ambaye ndio mgeni rasmi.
Amesema, mpaka sasa Halmashauri ya Jiji kupitia Idara ya Afya imewafikia wazee katika Kata 33 kati ya 41 na kuwapiga picha wazee wapatao 12,979 sawa na asilimia 66.41 ya wazee wote waliotambuliwa. Tayari wazee 10,290 wamepatiwa vitambulisho.
“Halmashauri ya Jiji katika kipindi cha kuanzia Mwezi Julai 2018 hadi Juni 2019, imetekeleza maelekezo ya serikali ya kutoa huduma ya matatibu bure kwa wazee ambapo jumla ya wazee 4,551 walihudumiwa katika vituo vya huduma vya Jiji wakitumia vitambulisho vya wazee,” ilieleza sehema ya taarifa hiyo.
Akizungumza na wazee hao kabla ya kuzindua rasmi baraza hilo, Katambi alitoa wito kwa jamii nzima kuwajali na kuwaenzi wazee kwani wamefanya kazi kubwa katika ujenzi wa Taifa na kuweka mazingira rafiki kwa vijana wa sasa kuishi kwa amani na utulivu.
“Wazee ni tunu ya Taifa, juhudi zao za muda mrefu ndiyo zimetufikisha hapa kama Taifa kwa hiyo ni lazima tuwaenzi kwa kila namna,” amesema Katambi.
Amesema, aliitaka jamii hasa vijana kuacha dhana potofu kuwa wazee wamepitwa na wakati, kwani kwa uhalisia vijana ndiyo waliopitwa na wakati kwa kuwa wazee walikuwepo tangu zamani na sasa wapo tofauti na vijana ambao wa kizazi kipya.
Leave a comment