BAADHI ya wazazi ambao watoto wao wamemaliza darasa la saba na kufaulu mitihani yao na kukosa nafasi za kujiunga na kidato cha kwanza wamemwomba Rais John Magufuli kuwafuta kazi wakuu wa mikoa ambao wameshindwa kuongeza vyumba vya madarasa. Anaripoti Dany Tibason, Dodoma … (endelea).
Wakizungumza na MwanaHALISI Online, wazazi hao walisema kuwa serikali imekuwa ikihamasisha elimu bure na kuwataka wazazi wasiopeleka watoto shule waadhibiwe lakini wakuu wa mikoa wameshindwa kuhamasisha ujenzi wa madarasa na kusababisha watoto kushindwa kujiunga kidato cha kwanza kutokana na kukosekana kwa madarasa.
Mmoja wa wazazi aliyejitambulisha kwa jina la Sophia Ally alisema kuwa serikali kitendo cha wanafunzi kushindwa kujiunga katika kidato cha kwanza licha ya kuwa wameshinda ni uzembe mkubwa wa wakuu wa mikoa iliyoshindwa kuwa na vyumba vya madarasa vya kutosha.
“Tumekuwa tukishuhudia walimu wakinyanyaswa na wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa kwa madai kuwa walimu hawatendi vizuri katika ufundishaji, lakini leo hii walimu wamejitahidi kuwafanya watoto wafaulu kwa wingi jambo la kusikitisha wanakosa kujiunga na kidato cha kwanza kisa kukosa madarasa.
“Tunamuomba Rais wetu msikivu, John Pombe Magufuli, kuwatumbua wakuu wa mikoa na wilaya ambao mikoa yao imeshindwa kuwapeleka watoto waliofahulu darasa la saba kushindwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa sababu ya kukosekana kwa vyumba vya madarasa,” alisema Sophia.
Naye, Yohana Digamile alisema kitendo cha wanafunzi kushindwa kujiunga kidato cha kwanza wakati wamefahulu ni dalili tosha za wakuu wa Mikoa na Wilaya kushindwa kutambua umuhimu wa elimu katika maeneo yao.
“Tunatakiwa kujiuliza baada ya Rais kuhimiza ununuzi wa madawati wakuu wa mikoa na wilaya walivyokuwa wakali sasa kwa hili hawakujua kuwa wapo wanafunzi wengi kuliko vyumba vya madarasa,je kwa mwaka jana wakuu hao wa mikoa na wilaya walionesha juhudi gani za kuomgeza madarasa,” alihoji Digamile.
Katika hatua nyingine baadhi ya wazazi hao walisema kama watoto wataendelea kutopata nafasi za kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za serikali licha ya kuwa wamefahuru basi hakuna haja yoyote ya serikali kuendelea kuhimiza elimu bure wala kuwawajibisha walimu ambao hawafanyi vizuri.
“Haiwezekani watoto 130,000 wakashindwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa kile ambacho kinadaiwa kuwa ni kukosekana kwa vyumba vya madarasa je sasa wazazi waanze kujenga vyumba hivyo vya madarasa, na kama walijiua hivyo kwanini wasingesema mapema kuwa watoto ni wengi mashuleni na vyumba vya madarasa havitoshi ili wazazi waanze kujenga wenyewe,” alisema Didamile.
Leave a comment