CHAMA cha Wavuvi Tanzania (TAFU), kimemtaka Rais Magufuli kuunda tume ya uchunguzi juu ya bei ya ununuzi wa samaki katika mikoa ya kanda ya ziwa kwani kuna viashiria vya ufisadi, anaandika Moses Mseti.
Frank Mwakimonga, mwenyekiti wa TAFU, ametoa ombi hilo leo wakati wa mazungumzo yake na baadhi ya wavuvi kuhusu sheria mpya ya uvuvi ikiwemo wavuvi kuanza kutumia bendera ya taifa katika mitumbwi na boti zao pamoja na kutumia leseni moja ya kuvua samaki, Sangara au Sato.
“Rais Magufuli anapaswa kuangazia katika raslimali ya uvuvi kwani wanunuzi wakubwa wa samaki wanaendelea kuiibia serikali.
“Tangu mwaka 1998 samaki aina ya Sangara na Sato bei yake imekuwa ikishuka kila kukicha na wavuvi wamekuwa wakinyonywa katika ununuzi tangu kipindi hicho,” amesema.
Sijaona James, msemaji wa chama hicho, amesema sheria mpya ya uvuvi inayotarajiwa kuanza kutumika kwa kutoa leseni maalumu za uvuvi itasaidia kuondokana na tatizo la uvuvi haramu nchini kwani mvuvi wa Sangara atavua Sangara pekee.
“Wafanyabiashara wakubwa wa samaki wamekuwa wakiwanyonya kwa kununha samaki kwa bei ndogo hivyo serikali inapaswa kuangalia namna ya kuwasaidia,” amesema.
Leave a comment