WATUMISHI wa Ofisi ya Bunge na Waziri Mkuu wameshauriwa kuwa na uelewa mpana kuhusu nafasi yao katika mchakato na mipango mbalimbali ili sera na sheria zitakazotungwa ziakisi na kujibu changamoto halisi zinazowakabili wananchi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Katibu wa Bunge, Stephen Kagaigai alisema hayo jana wakati akifungua mafunzo ya uchambuzi wa sera na matumizi ya tafiti kwa watumishi hao yaliyoandaliwa na Taasisi inayojishughulisha na utafiti katika masuala ya uchumi na maendeleo (REPOA).
Kagaigai alisema kati ya majukumu ya Bunge yaliyopo ni pamoja na kuishauri Serikali juu ya utungaji wa sera na sheria mbalimbali za nchi na kwamba bunge hujadili na kupitisha mipango ya Taifa, Bajeti ya serikali na hatimaye kuisimamia wakati wa utekelezaji.
Aidha Kagaigai alisema washiriki wa mafunzo hayo ni miongoni mwa washauri muhimu wa Bunge na Serikali wakati wa utekelezaji wa majukumu ya nchi ambapo mipango, sera na sheria zinazotungwa huzingatia maslahi ya wananchi.

“Kama wote mnavyofahamu, Tanzania ni nchi yenye Serikali iliyowekwa na wananchi na iko kwa ajili ya wananchi na inaangalia zaidi maisha na maslahi ya wananchi. Sera isiyozingatia uhalisia wa changamoto zinazowakabili wananchi itapelekea hatimaye kutungwa kwa sheria isiyofaa,” alisema Kagaigai.
Alisema ni muhimu washiriki hao wakawa na uelewa mpana na kufanya sera na sheria zinazotungwa zinaakisi au ziwe sawa na kujibu changamoto halisi zinazowakabili wananchi.
Alisema ni imani yake kuwa mafunzo hayo yatakuwa ni nyenzo muhimu ya kuwaongezea uelewa ili waweze kushauri mamlaka husika ipasavyo.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa REPOA, Dk. Donald Mmari alisema majukumu makubwa ya REPOA ni kufanya tafiti za kisera, kujenga uwezo wa watafiti katika masuala ya kisera na kufikisha matokeo ya tafiti hizo kwa watumiaji ikiwa ni pamoja na watunga sera na wafanya maamuzi juu ya mipango na mikakati ya maendeleo.

Alisema lengo kuu ni kuchangia katika juhudi za kuleta mabadiliko ya kijamii na kiuchumi ili kuwa na maendeleo jumuishi kama Dira ya Maendeleo endelevu (SDGs) na hata agenda ya Muungano wa Afrika 2063.
Dk. Mmari alisema katika kutekeleza mpango wa nne wa kimataifa wa miaka mitano (2020-24) wamedhamiria kuimarisha uhusiano kati ya tafiti na sera za nchi.
Alisema dhamira hiyo itafanikiwa kwa kushirikisha wadau mbalimbali wakati wa kuandaaa maeneo ya vipaumbele za tafiti zao sambamba na kuwa na program ya kuwajengea uwezo watafiti na watumiaji wa tafiti katika ngazi mbalimbali ambapo mafunzo hayo ni sehemu ya mpango huo.
Leave a comment