WATUMISHI 23 wa Kitengo cha Famasia cha Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), wanachunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwa tuhuma za kuandika taarifa za uongo katika mfumo wa utunzaji taarifa za kumbukumbu za utoaji dawa na vifaa tiba, na kusababisha upotevu wa dawa zenye thamani ya Sh.1.2 bilioni. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yanesemwa leo Jumatano tarehe 13 Januari 2021 na Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali John Mbungo, wakati anazungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Mbungo amesema, watumishi hao wanadaiwa kufanya udanganyifu huo kati ya mwaka 2018 hadi 2020.
Akielezea namna ubadhirifu huo ulivyofanyika, Mbungo amesema, watuhumiwa hao walikuwa wanaandika taarifa za uongo katika mfumo huo, kwa kuweka idadi kubwa ya vifaa vilivyotolewa tofauti na idadi halisi iliyotolewa kwa wateja na madaktari.
“Takukuru kwa kushirikiana na uongozi wa MOI, ilibaini dawa hizo zilichepushwa katika mfumo wa kutunza taarifa za kumbukumbu za utoaji dawa na vifaa tiba kwa wagonjwa wanaotibiwa,” amesema Mbungo.
Sambamba na hilo, watuhumiwa hao wanadaiwa kuongeza gharama kubwa katika bei tofauti na bei elekezi ya Serikali.
“Takukuru pia imebaini wako wafamasia huongeza bei na gharama kubwa kwa fomu za madaktari. Kutokana na ubadhirifu huo, dawa hizi zilikuwa zihujumiwe kwenye mfumo halali uliowekwa kwenye Serikali,” amesema Brigedia Mbungo.
Hata hivyo, Mbungo amesema, Takukuru kwa kushirikiana na MOI iliwahi kudhibiti ubadhirifu huo, baada ya kufanya uchunguzi.
“Takukuru kwa kushirikina na MOI yadhibiti uchepushaji na ubadhirifu wa dawa zenye Sh.1.2 bilioni ambazo zilichepushwa au hujumiwa kwa manufaa binafsi kwa watumishi wa kitendgo cha famasia,” amesema Mbungo.
https://www.youtube.com/watch?v=kGoyrRy1VJc
Amesema uchunguzi huo ulibainisha tofauti kati ya idadi ya dawa zilizotolewa na idadi iliyoandikwa katika mfumo huo.
“Ubadhirifu huu umedhibitiwa baada ya uchunguzi kubaini tofauti kati ya taarifa za dawa zilizoingizwa katika mfumo na taarifa zilizoandikwa na madatari katika fomu za wagonjwa waliohudumiwa,” amesema Brigedia Mbungo.
Mbungo amesema “Mfano daktari anandika dawa 30 kwa matumizi ya mgonjwa kwa muda wa mwezi 1. Mfamasia anaongeza dawa na kuingizia katika mfumo dawa 60 tofauti na alizoandika kwenye mfumo.”
Mbungo amesema watuhumiwa hao wanaendelea kuhojiwa na kwamba mahojiano yakikamilika hatua za kisheria zitafuatwa.
Leave a comment