SERIKLI imesema hadi kufikia tarehe 1 Septemba, 2021 jumla ya watumishi wa umma 174,222 wamepandishwa vyeo na kubadilishiwa mishahara yao. Pia imesema itaendelea kuboresha maslahi kwa watumishi wa umma kadri bajeti itakavyoruhusu. Anaripoti Victoria Mwakisimba TUDARCo … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 10 Septemba 2021, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Deogratius Ndejembi wakati akijibu swali la Mbunge wa Nyamagana, Stanslaus Mabula (CCM).
Mbunge huyo aliuliza ‘je, serikali ina mkakati gani wa kutimiza masharti ya ajira kwa watumishi ikiwa ni pamoja na kuwapandisha madaraja na stahiki zingine.
Akijibu swali hilo naibu waziri huyo amesema serikali imeendelea kutimiza masharti ya ajira kwa watumishi wake ikiwemo kuwapandisha vyeo watumishi ambapo serikali ilitoa barua kumb.Na.BC.46/97/03’D’/59 ya tarehe 28 Aprili, 2021 iliyoruhusu upandishwaji vyeo kwa watumishi wa umma kuanzia tarehe 1 Juni, 2021.
Pia ameeleza kwamba hadi kufikia tarehe 1 Septemba, 2021 jumla ya watumishi wa umma 174,222 wamepandishwa vyeo na kubadilishiwa mishahara yao.
Akiuliza swali la nyongeza mbunge huyo alihoji sababu za kuajiri vijana kutoka mataifa mengine pale ilihali kuna vijana wazawa ambao wanajitolea kufanya kazi kwenye taasisi mbalimbali hapa nchini.
Akijibu swali hilo Ndenjembi amesema serikali ina mpango mkakati wa kuwapatia fursa za ajira vijana hao na ndio maana hata wizara inapohitaji wafanyakazi matangazo yanatolewa ili kuwapa fursa vijana hao.
Aidha naibu waziri ametoa wito kwa vijana wote wanaojitolea kuandikisha majina yao kwenye serikali za mitaa.
Leave a comment