MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewaondolea hofu watumiaji wa mitandao ya simu wanaotaka kutumia huduma ya laini moja kwa mitandao yote kuwa hatawakosa huduma zinazotolewa na makampuni ya simu, anaandika Mwandishi Wetu.
Kaimu Naibu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Tehama, Mhandisi Nehemia Mwenisongole, alisema hayo mjini hapa jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Amesema huduma hiyo itakuwa ya hiari kwa watumiaji wa mitandao ya simu na itawasaidia kuondokana na kumiliki utitiri wa laini nyingi za simu na kutumia laini moja iliyobeba mitandao yote ya simu ambayo atahitaji kutumia.
“Ukiamua kuhamia kwenye mfumo huu wa kuunganishwa kutumia namba moja hakutakuwepo na madhara ya kuanza kuwaza kuwa wapo watu ambao nitawapoteza nikiingia huko,’’ alisema.
Aidha, amesema kuingia kwenye mfumo huo itasaidia kuondoa changamoto ya kukosekana kwa mtandao mahali mtumiaji atakapokuwa na kumsaidia kutumia mtandao mwingine utakaokua unapatikana eneo husika.
Amesema walianza kuingia kwenye mfumo huo wa mawasiliano kuanzia Machi mosi mwaka huu, ambapo alisema mchakato wa kuhamia mitandao mingine kwa kutumia namba moja hautazidi siku mbili.
Leave a comment