WATU watano wanaotuhumiwa kwa ujambazi, wameuawa katika majibizano ya risasi baina yao na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamesemwa leo Jumatatu tarehe 1 Machi 2021 na Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, wakati anazungumza na wanahabari.
Kamanda Mambosasa amesema, tukio hilo lilitokea tarehe 27 Februari 2021, maeneo ya Kivule Iranga, mkoani Dar es Salaam.
“Mnamo tarehe 27 Februari 2021, majira ya saa 12 asubuhi huko maeneo ya Kivule kwa Iranga, Jeshi la Polisi, Kanda Maalum Dar es Salaam kupitia kikosi chake cha kupambana na ujambazi lilifanikiwa kuwaua majambazi watano waliokuwa kwenye gari namba T 836 DHF aina ya Toyota Noah,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda huyo wa Polisi Dar es Salaam amesema, tukio hilo lilitokea baada ya polisi kuwawekea mtego watuhumiwa hao, ambao uliwawezesha kuzuia mipango yao ya uhalifu.
Baada ya Polisi kufanikiwa kudhibiti tukio hilo, watuhumiwa hao wa ujambazi waliokuwa sita, walianza kuwarushia risasi polisi, ndipo majibizano hayo yalipozuka na kusababisha vifo vya watu watano.
“Majambazi hao wapatao sita, wakiwa kwenye gari hiyo kwenda kufanya uhalifu maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam, lakini kabla hawajatimiza lengo lao, kikosi kazi cha Jeshi la Polisi kiliweka mtego na kufanikiwa kuzuia ujambazi huo kwa kutaka kuwakamata wahalifu hao,” amesema
“Lakini majambazi hao, walitoka kwenye gari na kuanza kukimbia huku wakiwarushia askari risasi na hatimaye askari walijibu mapigo na kufanikiwa kuwapiga risasi majambazi watano ambao walifariki dunia papo hapo.”
“Jambazi mmoja kufanikiwa kukimbia huku akifyatua risasi hovyo na kumjeruhi askari mmoja,” amesema Mambosasa.
Mambosasa amesema, baada ya watuhumiwa hao kupekuliwa, walikutwa na bastola moja ikiwa na risasi tatu ndani ya magazine na maganda mawili ya bastola.
Amesema miili ya watuhumiwa hao imeifadhiwa Hospitali yaTaifa Muhimbili.
Leave a comment