JUMLA ya watu 17 wamepoteza maisha katika klabu moja ya usiku iliyopo katika Mji wa London Mashariki nchini Afrika Kusini, kutokana na hali iliyodaiwa kuwa ni mkanyagano. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumzia tukio hilo leo tarehe 26 Juni, 2022 Msemaji wa polisi katika eneo hilo, Tembinkosi Kinana amesema miili ilipatikana katika ukumbi wa Enyobeni Tavern leo mapema huku wengine kadhaa wanadaiwa kujeruhiwa.
“Hali katika eneo la tukio hilo inachunguzwa, hatutaki kutoa taarifa za uvumi wowote katika tukio hili,” amesema.
Aidha, inaelezwa kuwa waathirika wa tukio hilo walikuwa wakisherehekea kumaliza mitihani ya elimu ya juu nchini humo.
Licha ya wazazi na ndugu jamaa waliopatwa na mkasa huo, kuzuiwa kuiona miili hiyo, inadaiwa wamekusanyika katika eneo la tukio na kutaka ukumbi huo kufungwa.
Idadi kubwa ya wafanyakazi wa huduma ya dharura wako kwenye eneo la tukio katika jimbo la Eastern Cape.
Brigedia Kinana aliwaambia waandishi wa habari wengi wa waliokutwa wamekufa ni vijana wenye umri kati ya miaka 18 na 20.
Walioshuhudia waliambia gazeti la Daily Dispatch kwamba miili ilikuwa ndani ya ukumbi huo kana kwamba imeanguka sakafuni.
Leave a comment