WADAU wanaotoa msaada wa kisheria kwa wananchi, wameiomba Serikali itenge ruzuku kwa ajili ya kuwezesha shughuli hizo ili ziwe endelevu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Ombi hilo limetolewa mwishoni mwa wiki, kupitia maazimio ya wadau walioshiriki kongamano la msaada wa kisheria la 2022, jijini Dodoma.
Akisoma maazimio hayo, Mratibu wa Mtandao wa Watoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria nchini (TAPANET), Tolbert Mmassy alisema ombi hilo linalenga kuboresha sejta ya msaada wa kisheria.
Mbali na ombi la ruzuku, Mmassy alisema wadau hao wanaomba wasaidizi wa kisheria kwa kila ngazi watambulike ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
Maombi mengine yaliyotajwa na Mmassy ni, watoa huduma za msaada wa kisheria wapewe ofisi katika majengo ya umma, ili kuwasaidia watu wengi wenye uhitaji, utekelezaji wa shughuli za huduma hizokwa kushirikiana na Serikali, ili kuongeza wigo wa huduma za msaada wa kisheria kwa wadau mbalimbali.
Mengine ni, watoa huduma za msaada wa kisheria wajengewe uwezo kwenye mifumo na sheria jinai, pamoja na Serikali kutenga ruzuku maalumu katika kutoa msaada wa kisheria ili kuhakikisha kuwa huduma hizo zinakuwa endelevu.
Akifunga kongamano hilo, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria nchini Tanzania, Geofrey Pinda, alisema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wadau wanaotoa msaada wa kisheria kwa wananchi.
“Ni muhimu sisi kama Wizara kutathimini thamani ya utoaji wa msaada wa kisheria na kuimarisha huduma za msaada wa kisheria nchini, kwa kujengea uwezo watoa huduma wa msaada wa kisheria. Na ndio mana sisi kama Wizara tukaona ni vyema kuondoa vikwazo kama vile ada ya mwaka kwa wasaidizi wanaojitolea bila malipo yoyote na kuendelea kuboresha huduma hizi nchini,” alisema Pinda.
Pinda aliwataka wadau kuendelea kushirikiana na Serikali, hasa kwenye utekelezaji wa sera, sheria, masuala mbalimbali ya haki ambayo yanawahusu wananchi.
“Nina amini ili kuwepo matunda mazuri, kunahitajika uhusiano endelevu kati ya serikali na wadau wa sekta ya msaada wa kisheria. Kwa kutambua hilo, nawahakikishia kuwa ofisi yangu itakuwa wazi kufanya kazi na nanyi kwa kupokea taarifa, ushauri na mazungumzo mengine muhimu kuhusu mambo yanayowakabili wananchi katika sekta hii nyeti nchini,” alisema Pinda.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Legal Services Facility (LSF), Lulu Ng’wanakilala, ambao ndiyo waandaaji wa kongamano hilo kwa kushirikiana na Wizara ya Katiba na Sheria, alisema kupitia kongamano hilo la siku mbili, wadau walijadili kwa kina masuala yahusuyo sekta hiyo.
“Kikao hiki kimetupa maazimio mengi. Niahidi kuwa, wataalamu wetu wamerekodi yote yaliyojadiliwa na wadau. Baada ya kongamano hili timu hiyo itaandaa taarifa rasmi kwa ajili ya kuiwasilisha serikalini ili ifanyiwe kazi kwa ajili ya kuboresha na kuongeza ufanisi wa sekta ya msaada wa kisheria nchini” alisema Ng’wanakilala.
Vilevile, Ng’wanakilala ameishukuru Serikali chini ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa ushirikiano wao, katika kuhakikisha inatoa mafunzo kwa watoa huduma za msaada wa kisheria na kuongeza kiwango cha upatikanaji wa huduma hizi kwa wanawake na watoto, ambao ndio wahanga wakubwa na vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu.
Leave a comment