SHIRIKA linalosimamia haki za watetezi wa haki za binadamu Afrika (Defend Defenders), Kwa kushirikiana na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania .(THRDC), unafanya warsha ya kujadili mazingira ya watetezi wa haki za binadamu nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Warsha hiyo iliyoanza tarehe 7 Hadi 10 Desemba 2022, inafanyika jijini Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na watetezi wa haki za binadamu kutoka mashirika wanachama wa THRDC.
Akifungua warsha hiyo, Mwenyekiti wa Defend Defenders, Hassan Shire amesema inafanyika Kwa mara ya pili nchini Tanzania, (mara ya kwanza ilifanyika 2012), ili kujua pengo na mahitaji yanayohitajika Kwa ajili ya kuwalinda watetezi wa haki za binadamu nchini.
“Miaka 10 iliyopita tulikuwa hapa jijini Dar es Salaam na Sasa tunafanya claiming space ya pili Kwa ajili ya watetezi wa haki za binadamu kujua pengo na mahitaji katija kuwalinda watetezi wa haki za binadamu,” amesema Shire.
Amesema majadiliano yatakayofanyika Yana lengo la kujenga mtandao, umoja na uwajibikaji katika mazingira wanayokutana mayo watetezi wa haki za binadamu Tanzania katika kuchochoea uwajibikaji, uwazi na utawala wa Sheria Tanzania.
Shire amesema, zinafanyika jitihada kuhakikisha kwamba nchi 11 zinajiunga na Defend Defenders, ikiwemo Eritrea na Rwanda.
Aidha, Shire amesema anajua kwamba Rais Samia Suluhu Hassan, atakuwa mtetezi namba moja wa haki za binadamu Tanzania, kwa kuwa amekuwa mtetezi wa haki mbalimbali ikiwemo za mazingira.
Amesema, hakuna ubishi kwamba Kuna changamoto zinazowakabili watetezi wa haki za binadamu, ikiwemo changamoto za kisiasa, rushwa, ukosefu wa ulinzi, uwajibikaji na uwazi.
Naye Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, amesema warsha hiyo imelenga kudai mazingira Bora ya watetezi wa haki za binadamu Tanzania ambapo washiriki watajifunza masuala mbalimbali kuhusu masuala yao.
Pia, katika warsha hiyo kutakuwa na maadhimisho ya siku ya haki za binadamu na mkutano mkiu wa watetezi was haki za binadamu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCONGO), Dk. Lilian Badi, amewaahidi watetezi wa haki za binadamu kwamba wataendelea kuwapa ushirikiano ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi zaidi ikiwa pamoja na kuondoa changamoto zinazowakabili.
Aidha, Dk. Lilian amezitaka NGO’s kufanya kazi Kwa mujibu wa Sheria na maslahi ya nchi.
“Tunataka wanapotoka hapa kwenda kutekeleza mbinu wanazofundishwa wasikiuke Sheria za nchi, tunatambua Serikali ni sikivu tukiomba inatusikia na kutekeleza. Zinatakiwa kushirikiana na Serikali katika kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” amesema Dk. Lilian.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Patience Mtwina, amesema tume hiyo itaendelea kushirikiana na watetezi wa haki za binadamu nchini, Ili watekeleze majukumu Yao Kwa ufanisi huku akiwataka wafuate Sheria na miongozo ya nchi.
Leave a comment