ADHABU iliyotolewa na Kamati ya Maadili ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kwa Televisheni ya Mtandaoni ya Watetezi TV ya faini ya Shilingi 5 milioni imebatilishwa. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Uamuzi wa kubatilisha adhabu hiyo umetolewa leo Jumatatu tarehe 4 Mei 2020 na Baraza la Ushindani (FCT) kutokana na rufaa iliyokatwa na televisheni hiyo.
Televesheni hiyo ambayo ipo chini ya Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binaadamu Tanzania (THRDC) haikuridhishwa na adhabu hiyo waliyopewa.
Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania iliwatoza Watetezi TV faini ya Shillingi millioni 5 kwa kutokuweka sera au mwongozo wa watumiaji kinyume na Kanuni ya 5(1)(c) ya Kanuni za Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta (Maudhui ya Mtandaoni), 2018.
Kamati ya Maudhui ya TCRA klifikia uamuzi huo kulingana na Kanuni ya 18 ya Kanuni za Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta (Maudhui ya Mtandaoni), 2018.
Watetezi TV haikuridhika na uamuzi huo na hivyo wakakata rufaa mbele ya Baraza la Ushindani kwa sababu tatu; Mosi, kwamba kamati ya Maudhui ilikosea kisheria kwa kutumia kifungu kisichosahihi kufikia uamuzi wake. Pili, kwamba Kamati ya Maudhui ilitenda bila kuwa na mamlaka na tatu, kamati ilikosea kisheria kwa kushitaki chombo kisichokuwepo.
FCT imetoa uamuzi wake kwenye rufaa iliyokatwa na Watetezi TV tarehe 27 Septemba 2019 ya kupinga adhabu ya Kamati ya Maudhui ya TCRA.
Mwananchama wa FCT, Dk. Theodora Mwenegoha, amesema Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TRCRA) haina mamlaka ya kutoza faini chini ya Kanuni ya 18 ya Kanuni za Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta (Maudhui ya Mtandaoni), 2018.
“Baraza limefikia uamuzi wa kuweka kando uamuzi uliotolewa na Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano na kubadilisha adhabu kuwa kulipa faini ya shilingi Millioni Tatu (3,000,000) chini ya kifungu cha 44(2)(b) cha Sheria ya Mamlaka ya Mawasiliano.”
“Baraza limeeleza kifungu sahihi cha Sheria lilichopaswa kutumika ni kifungu cha 44(2)(b) cha Sheria ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania. Hata hivyo, kifungu cha 44 pia kinakosa viungo muhimu vya kuzingatiwa kabla ya kutoza faini,” amesema Dk. Mwenegoha.
Hivyo, faini yoyote iliyotozwa na Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasilano Tanzania haikuwa sahihi kulingana na Kanuni ya 18 na hivyo inapaswa kupingwa mbele ya mamlaka husika kama Baraza la Ushindani.
Mawakili waliiwakilisha Watetezi TV kwenye rufaa hiyo ni pamoja na Benedict Ishabakaki, Bertha Nanyaro na Rayson Elijah Luka.
Leave a comment