WATENDAJI wa kata, mitaa na vitongoji na maofisa afya wote ndani ya Jiji la Dodoma wametakiwa kuhakikisha wanasimamia usafi wa mazingira ambao unafanyika kila siku ya jumamosi na watakaoshindwa wataripotiwa kwa mkurugenzi wa jiji kwa ajiLi ya hatua za kinidhamu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa tarehe 24 Machi 2023 Jijini Dodoma Afisa Mazingira wa Jiji Dickson Kimaro kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji, amesema kuwa kila mtendaji wa kata, mtendaji wa mtaa, mtendaji wa kitongoji na maafisa afya wote wanatakiwa kuhakikisha wanasimamia usafi wa mazingira katika maeneo yao.
Aidha ameelekeza kuwa kila mkazi wa jiji la Dodoma anatakiwa kufanya usafi katika maeneo yake na kusafisha mitaro ya maji ya mvua iliyopo karibu na maeneo ya makazi anapoishi.
Pia amesema kuwa wafanyabiashara wote na wakazi wanaoishi kandokando mwa barabara kuu za Arusha, Iringa road, Dar es Salaam na Singida kuhakikisha wanaokota taka na mifuko ya plastiki kandokando mwa barabara.
“Ni marufuku kwa kampuni au kikundi chochote cha usafi kutupa takataka ovyo, aidha mnatakiwa kushiriki kufanya usafi wa barabara za mitaa mnaofanya kazi.
“Kila mtendaji wa kata ahakikishe watendaji wa mitaa na maafisa afya walioko katika kata wanasimamia usafi wa kila Jumamosi na wale watakaoshindwa kusimamia usafi huo wataripotiwa kwa Mkurugenzi wa Jiji kwa hatua zaidi za kinidhamu” ameeleza Kimaro.
Sambamba na hilo Kimaro amesema kuwa itumiwe Polisi Jamii na Mgambo kutoza faini kwa wanaoharibu na kuchafua mazingira na fedha hizo zitumike kwa shughuli za usafi hususani kulipa ngambo na kununulia vifaa vya usafi.
Leave a comment