WANAKIJIJI wa kijiji cha Mtipule kilichopo kata ya Msongozi wilayani Mvomero mkoani hapa wameyatelekeza mashamba yao kwa takribani miaka minne mfululizo wakihofia kuvamia na kuuawa na tembo waharibifu, anaandika Christina Haule.
Mwenyekiti wa kijiji hicho, Luanda Kalunga amesema wanakijiji hao walitelekeza mashamba yao tangu mwaka 2012- 2015 kufuatia Tembo kula na kuharibu mazao yao kila msimu wa kilimo.
Kalunga alikuwa akizungumza katika semina ya kuimarisha ushiriki wa jamii kwa kutunza makazi ya Tembo katika hifadhi ya Taifa ya Mikumi kwenye mradi uliofadhiliwa na mfuko wa misaada wa Uingereza ujulikanao kama The Rufford Foundation (RSG) na unaofanyika kijijini hapo.
“Wakulima wa kaya 48 za kijiji chetu, walitelekeza mashamba yao kwa miaka minne kwsababu Tembo walikuwa wakivamia na kuwajeruhi wananchi huku wakiharibu mazao wanayoyakuta mashambani ambapo mpaka sasa tayari wameshawauwa watu wawili na kumjeruhi mmoja.
“Waliouawa na Tembo ni pamoja na Josephat John na Emmanuel Valentino ambao wote ni wakulima lakini pia yupo mkulim ninayemkumbuka kwa jin moja la Kazulege, hadi sasa anatumia mipira kupata haja ndogo,” amesema.
Mwenyekiti huyo amesema ana matumini kuwa wakulima watarejea katika mashamba yao watakapopata elimu ya kukabiliana na Tembo kwa kuweka mizinga ya nyuki itakayomfanya Tembo kutopita shambani na kula au kufanya uharibifu wowote.
Ameeleza masikitiko yake juu ya wananchi wanaoharibiwa mazao yao kutolipwa fidia akisema; “Kijiji chetu kipo jirani na hifadhi ya Taifa ya Mikumi, Tembo wanaoharibu mazao yetu na tunajazwa kwenye malipo ya fidia lakini kila mwaka hatulipwi.”
Angelus Runji meneja wa mradi huo, alisema kuwa kufuatia kupata mradi huo wa miezi minane kwenye vijiji vitano vya wilaya za Mvomero na Kilosa watawaelimisha wananchi ili kuondoa dhana mbaya ya wakulima kumchukia Tembo badala yake wamtunze na kumlinda.
“Jamii ya vijiji hivi inaona uwepo wa Tembo ni sawa na janga au shida kubwa tofauti na malengo na matakwa ya Serikali juu ya uhifadhi na ulinzi wa Tembo kama Rasilimali ya Taifa, ni lazima sasa ielimishwe juu y umuhimu wa maliasili zetu ikiwemo wanyama,” amesema Runji.
Leave a comment