POLISI Mkoa wa Kilimanjaro nchini Tanzania linawashikilia watu watatu akiwemo mtoto wa miaka 16 kwa kosa la kukutwa wakisafirisha bangi (salphet) 15 zenye uzito wa kilogram 379 na misokoto 88 ya bangi ikitokea Moshi mjini kwenda nchi jirani ya Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa tarehe 17 Julai 17,2020 ,Kamanda wa polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Emmanuel Lukula amesema tukio hilo limetokea jana jioni Alhamisi maeneo ya njia panda baada ya gari lenye usajili wa namba T.802 AFZ Toyota hiace linalofanya safari zake kutoka Moshi mjini kwenda Holili kukutwa limepaki pembezoni mwa barabara.
”Jana askari polisi wakiwa doria, waliona gari hilo likiwa limepaki pembezoni mwa barabara ndipo walisogea mpaka eneo gari hilo lilipokuwa na kumkuta dereva wa gari hilo, Mosses Palanjo (44) akiwa anahangaika kuliwasha gari hilo ambapo katika ukaguzi wao ndipo walipogundua kuwepo kwa mizigo hiyo ya bangi,”amesema Kamanda Lukula
Aidha Kamanda Lukula amewataja wengine waliokamatwa na bangi ni Zubeda Ally (40) mkazi wa Kolila Kia na mtoto wake mwenye umri wa miaka 16, Emmanuel Joel wakiwa na bangi misokoto 88 ndani ya nyumba yao wanayoishi.
Kamanda Lukula amesema hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watuhumiwa hao kwa kukutwa na bangi kinyume cha sheria.
Leave a comment