WATANZANIA wawili wamepandishwa kizimbani kwa wakikabiliwa na mashtaka ya kumtumia mlemavu kujitajirisha kupitia kwa kuombaomba katika barabara za jijini Nairobi nchini Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Washtakiwa hao, Kuyi Paulo na Sita Yohana walifikishwa katika Mahakama ya Milimani Jumatatu tarehe 30 Agosti, 2021 wakituhumiwa na ulanguzi wa binadamu.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini humo, wawili hao pia wanaripotiwa kumpokonya mlemavu huyo pesa alizokuwa anaombaomba barabarani jijini Nairobi.
Hata hivyo, wawili hao walikanusha shtaka la kukiuka haki za mlalamikaji huyo mwenye umri wa miaka 14.
Mahakama pia ilifahamishwa kuwa wawili hao walikandamiza haki ya mlalamishi kwa kumnyima fursa ya kupata elimu ili wajikimu kiuchumi.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Milimani, Zainab Abdul alielezwa na Kiongozi wa Mashtaka, Everlyn Ongunga kuwa wawili hao walikuwa wakimsafirisha mlemavu huyo kila siku katika mtaa Shauri Moyo, Nairobi kuomba kando ya barabara.
Hakimu Abdul aliwashurutisha wawili hao kulipa dhamana ya Sh milioni 6.3 pesa taslimu kila mmoja.
Leave a comment