WIZARA ya Nishati wakati Tanganyika (Tanzania Bara) inapata uhuru mwaka 1961 ni mikoa miwili pekee ndiyo iliyokuwa na nishati ya umeme ikilinganishwa na sasa ambazo zaidi ya watanzania milioni 47 katika mikoa yote wamepata umeme. Anaripoti Danson Kaijage – Dodoma… (endelea)
Hayo yameelezwa leo tarehe 9 Novemba, 2021 jijini Dodoma na Naibu Katibu Mkuu wa Nishati, Mhandisi Felichesm Mramba wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio wizara yake kwa kipindi cha miaka 60 tangu uhuru ulipopatikana.
Mramba ameitaja mikoa hiyo iliyokuwa na umeme kuwa ilikuwa Tanga kwa kuwa kipindi hicho ulikuwa unazalisha zao la mkonge ilihali Dar as salaam ulikuwa na uhitaji wa umeme kwa ajili ya usafiri wa treni.
Kwa upande wa mafuta na gesi Mramba amesema katika kipindi cha mwaka 2004 hadi Juni, 2020 matumizi ya gesi asilia ya Mnazi Bay na Songo Songo yamesaidia Serikali kuokoa zaidi ya Shilingi trilioni 38 ambazo zingetumika kwa ajili ya ununuzi wa mafuta ya mitambo ya umeme na ya viwandani.
Aidha, ameeleza kuwa hadi Juni, 2021 zaidi ya magari 750 yamewekewa mfumo wa matumizi ya nishati ya gesi asilia.
Aidha, amesema Wizara ya Nishati imeendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Mpango Mkakati wa Wizara wenye malengo makuu sita.
“Malengo hayo ni pamoja na kuongeza uzalishaji wa umeme na kuboresha mifumo ya usafirishaji na usambazaji wa umeme, kuongeza mchango wa nishati jadidifu katika matumizi mbalimbali ya nishati na kuimarisha shughuli za utafiti na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia.
“Mengine ni kuboresha rasilimali za Wizara ili kutoa huduma bora za nishati, kutekeleza kwa ufanisi Mkakati wa Taifa wa Kupambana na Kuzuia Rushwa na Kupunguza maambukizi ya VVU na UKIMWI na, kusimamia Sekta ya Umeme na Nishati Jadidifu, Sekta ya Mafuta na Gesi” amesema Mramba.
Akizungumzia mafanikio yaliyopatikana katika Sekta ya Umeme na Nishati Jadidifu, Mramba amesema ni pamoja na kuongezeka kwa uzalishaji wa umeme nchini.
Amesema hadi kufikia mwezi Septemba, 2021 upatikanaji wa umeme umefikia Megawati (MW) 1,609.91 ikilinganishwa na MW 17.5 kabla ya uhuru.
Ameeleza kuwa mahitaji ya juu ya umeme nchini yamefikia MW 1,273.42 mwezi Oktoba, 2021.
“Uwezo wa mitambo ya kufua umeme iliyoungwa katika mfumo wa Gridi ya Taifa umefikia MW 1,573.65 ambapo umeme wa nguvu ya maji ni asilimia 36.46, gesi asilia 57.28, mafuta 5.60 na tungamotaka (Biomass) asilimia 0.67” ameeleza.
Leave a comment