MKURUNGEZI wa halmashauri ya manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi ametangaza vita kwa wamiliki wa viwanja vikubwa ambao wameshindwa kuviendeleza kwa zaidi ya miaka mitatu, anaandika Dany Tibason.
Kunambi amesema wamiliki hao wasipoviendeleza watawanyang’anya na kuwapatia wananchi wanyonge.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma Kunambi amesema wamiliki wote wenye viwanja vikubwa na zaidi ya kimoja wamepewa muda wa siku 90 tangu sasa wawe wameisha viendeleza vinginevyo vitatwaliwa kwa mujibu wa sheria ya ardhi.
“Kwa wale ambao walipewa barua ya viwanja lakini hawajafanya malipo nao wamepewa muda wa siku 30 kuanzia sasa vinginevyo viwanja hivyo vitachukuliwa kwa mujibu wa sheria,” amesema
Kunambi ambaye ameonekana kujitapa katika utendaji wake wa kazi tangu kuvunjwa kwa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA), amesema kuwa hakuna mtu hata mmoja ambaye ataonewa katika kutekeleza suala zima na upangaji wa mji wa Dodoma.
Kunambi amesema wananchi wote ambao wameshindwa kuendeleza maeneo yao kwa muda wa zaidi ya miaka mitatu maeno hayo yatachukuliwa kwa mujibu wa sheria na kupewa watu ambao ni wahitaji wa viwanja.
Akizungumzia kuhusu wageni ambao wamekuwa wakinunua viwanja kwa madalali, Kunambi amewataka wateja wote wanaotaka kununua viwanja wafike katika ofisi ya mkurugenzi ili kupata viwanja vya uhakila kwani wasipofanya hivyo watatapeliwa.
Akizungumzia kitendo cha Manispaa kukusanya mapato na kuvuka lengo amesema katika mwaka wa fedha 2016/17 wamevuka lengo na kufikia asilimia 117.
Hata hivyo, ameshindwa kutoa takwimu ni kwa kiwango gani amewawezesha akina mama na vijana kwa kuwapatia fedha za maendeleo ambazo zinatakiwa kutolewa na halmashauri.
Leave a comment