Thursday , 28 March 2024
Home Habari Mchanganyiko Washukiwa wa unga, wamtii Makonda
Habari MchanganyikoTangulizi

Washukiwa wa unga, wamtii Makonda

Wema Sepetu akiwasili kituo cha Polisi cha Kati
Spread the love

WEMA Sepetu amefika. Babuu wa Kitaa amefika. Khalid Mohamed (TID) amefika. Hamidu Chambuso (Nyandu tozi) naye amefika. Ni wasanii walioepuka ‘kiaina’ mgogoro mkubwa na serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam, chini ya Paul Makonda, anaandika Faki Sosi na Pendo Omary.

Wametii amri ya Mkuu wa Mkoa (RC) Makonda ambaye jana kupitia vyombo vya habari, alitaka wasanii kadhaa wa filamu na muziki nchini waripoti kituo kikuu cha polisi (Central) kuhusiana na ushiriki wao katika matumizi au biashara ya dawa za kulevya (unga).

Orodha ya Makonda ilikuwa na wasanii wanane, lakini wale walioshindwa kufika, ni kama wamejitafutia mgogoro na serikali. Sasa inalazimu kusakwa na kukamatwa na kulazwa mahabusu.

Wema ni muigizaji na Miss Tanzania 2006, Babuu wa Kitaa ni mtangazaji kituo cha televisheni cha Clouds, TID na Chambuso ni waimbaji wanaotamba katika muziki wa kizazi kipya, Bongofleva.

Katika tukio la kujisalimisha kwao mbele ya Makonda na Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro, leo makao makuu ya jeshi hilo jijini, wasanii hao walihojiwa kwa ajili ya kile kilichoitwa “uchunguzi zaidi wa tuhuma dhidi yao.”

Lakini kwa wale walioshindwa kufika, Makonda ameamuru wasakwe. “Kuna watu (wasanii) tuliwaita. Baadhi tumeambiwa hawajafika. Hawa tumeamuru wakamatwe (haraka) leoleo, wawekwe ndani hadi Jumatatu,” amesema Makonda katika tukio lililokuwa likioneshwa moja kwa moja na baadhi ya vyombo vya habari.

Tangazo hili jipya, linamaanisha kuwa Rashid Makwilo (Chid Benz), Heri Samir (Mr. Blue) na Rachel maarufu kama Rachel Kizunguzungu, ni miongoni mwa wasanii walioanza kusakwa kwa kutotii amri ya kujisalimisha.

Kama vile hiyo haikutosha, orodha ya wasanii wanaochunguzwa kwa tuhuma za kushiriki mihadharati (unga), imetuna leo, baada ya kutajwa kwa wengine akiwemo Vanessa Mdee au Vee Money, msanii maarufu anayetamba kwenye luninga, pamoja na Tunda ambaye ni mrembo anayeshiriki kupendekeza muziki kwenye video za wasanii.

“Waliofika muda si mrefu tutakaa nao ndani na kuwahoji. Hata hivyo bado tunaendelea na uchunguzi. Na wengine wanaotakiwa kufika polisi ni wasanii Vanessa Mdee na Tunda,” amesema Makonda.

RC Makonda amedai kuwa hatua aliyochukua imefurahisha wananchi wema wa Dar es Salaam kiasi kwamba baadhi yao, “tayari wamenipatia majina mengine ya askari watatu na watu wengine (raia) watano wanaojihusisha na biasahara haramu ya dawa za kulevya.”

“Wamo askari wengine kwa majina ya Mudi Zungu, Fadhili na Ben, hawa waunganishwe na mali zao zipo,” amesema.

Amesema mwingine ambaye hakumtaja, ameanza kuhangaika kuuza nyumba yake eneo la Kigamboni. Akamtaja Omary Sanga, aliyedai kuwa ni mfanyabiashara maarufu wa dawa za kulevya ambaye pia ametambulisha kama mmoja wa watu waliosababisha vijana wengi wa Kitanzania kufungwa nchini China.

“Nimepata taarifa kuwa (Sanga) anajiandaa kutoka Dubai kwenda China,” amedai RC Makonda.

Kamishna Sirro amesema tayari hatua kuhusu askari 12 wa Jeshi la Polisi waliotajwa na mkuu wa mkoa kwa tuhuma za kushiriki biashara ya dawa za kulevya, zimeanza kuchukuliwa.

“Kati ya askari 12 waliotajwa, wawili walishahama kikazi, hawapo mkoa wa Dar es Salaam, tayari askari saba wamefika hapa kutii amri na wengine watatu tunawatafuta,” amesema Kamishna Sirro.

Hatua hii mpya ya RC Makonda imezua mjadala mpana na kusukuma watu wengi kushiriki kujadili kupitia mitandao ya kijamii. Wapo wanaoona ni dhihaka kwa kuwa washiriki wakuu wa kuingiza mihadharati hawajaguswa “japo wanajulikana.”

“Muda mrefu huko nyuma umma ulifahamishwa kuwa orodha ndefu ya wafanyabiashara wakubwa wa unga imekabidhiwa mikononi kwa Rais. Tunajua ni rais aliyepita (Dk. Jakaya Kikwete) lakini si alikabidhi mafaili yote ya masuala yaliyokuwa mikononi mwake na sasa kuwa ni jukumu la kiongozi aliyemrithi,” anahoji mkazi wa Kinondoni aliyezungumza na ripota wa MwanahalisiOnline.

 

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

Habari za SiasaTangulizi

CAG aibua madudu halmashauri 10, TANESCO na MSD

Spread the loveRIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali...

error: Content is protected !!