WANAVIJIJI wa Kata ya Bukumi, wilayani Musoma Vijijini, Mkoa wa Mara, wamejenga maabara tatu za masomo ya sayansi katika Shule yao ya Sekondari Mtiro, ambayo wanafunzi wake wameikosa huduma hiyo kwa miaka 17 tangu ilipoanzishwa 2006. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 11 Machi 2023 na Ofisi ya Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo, wanavijiji hao wamepanga kufanya ujenzi wa maabara hizo katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia tarehe 13 Machi mwaka huu.
“Tarehe 9 Machi 2023, Prof. Muhongo aliendesha harambee shuleni hapo kwa lengo la kupata fedha za ujenzi wa maabara tatu za masomo ya fizikia, kemia na bailojia za Mtiro Sekondari, matokeo yake fedha zilizochangwa taslimu ni Sh. 494,000, ahadi Sh. 4.49 milioni, saruji mifuko 26 na mchanga roli Tano,” imesema taarifa hiyo.
Ofisi hiyo imesema kuwa, Prof. Mujongo ameanza kuchangia ujenzi huo kwa kutoka mifuko 150 ya saruji.
Imesema ujenzi wa maabara hizo unatarajiwa kukamikika Juni, 2023.
Imesema shule ya Sekondari Mtiro Ina wanafunzi 682, ambapo 42 pekee ndiyo wanasoma masomo ya sayansi, huku ikiwa na walimu 17, wanne kati yao ni wa kujitolewa huku 13 wakiwa waajiriwa serikalini.
Kupitia taarifa hiyo, Prof. Muhongo amewataka wadau wengine wa maendeleo kutoa michango yao Kwa ajili ya kuwezesha ujenzi wa miundombinu ya elimu jimboni humo.
Leave a comment