MKUTANO wa wadau wa vyama nchini Tanzania, unatarajiwa kufanyika tarehe 21 Oktoba 2021, jijini Dodoma. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo ilitolewa jana Jumatatu tarehe 20 Septemba 2021 na Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam, kuhusu ratiba ya mkutano huo wa wadau.
Jaji Mutungi alisema, mkutano huo utakutanisha wadau wa siasa, ikiwemo Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro na wawakilishi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), ambao utaongozwa na mtu asiyekuwa na upande wowote, ili kuweka usawa.
“Kikao cha wadau kikiendeshwa na IGP kinaweza leta taswira IGP huyo huyo ndiyo tunamlalamikia, kikiendeshwa na msajili, msajili huyo huyo tuna madudu yake tunataka kuyasema, mwenyekiti wa uendeshaji kikao atakuwa mtu neutral,” alisema Jaji Francis.
Msajili huyo wa vyama vya siasa alisema, kikao hicho kitasaidia kupatikana kwa muafaka wa vikwazo, vinavyokabili wadau wa siasa na demokrasia nchini.
“Naamini huu mlolongo tuliyouweka utavuka vikwazo vyote, ambavyo vilifikirika kwamba vitakwamisha muafaka mzuri tunaotaka upatikane na nieleweke vizuri, ninaposema muafaka kuna vitu ambavyo kama viko kisheria hakuna suala la muafaka si sheria ipo?” alisema Jaji Mutungi.
Jaji Mutungi alisema “lakini sisi tunataka kuangalia kama sheria ipo, lakini sisi tunataka tuangalie kama sheria ipo halafu bado kuna misuguano tatizo liko wapi. Ndiyo mantiki ya watu kukaa meza moja kuelewana.”
“Umuhimu wa kukaa ndiyo dhana nzima ya demokrasia, tunapofika mahala tukajaribu kuona kwamba hapa mbona kuna sintofahamu, inawezekana ni sintofahamu ya kuelimishana tu, ya kueleweshana,” alisema Jaji Mutungi.
Jaji Mutungi alisema mkutano huo wa wadau utatanguliwa na vikao mbalimbali, ikiwemo kikao cha ofisi yake na Jeshi la Polisi, kitakachofanyika jijini Dodoma, tarehe 23 Septemba 2021, kikifuatiwa na kikao cha Kamati ya Uongozi ya Baraza la Vyama vya Siasa, kitakachofanyika tarehe 30 Septemba 2021.
“Tutakaa na na Polisi halafu tutaitisha kamati ya uongozi ya baraza, sababu imeonekana tusiongee tu na Polisi na wanasiasa tuwape kikao maalum, wakae warasimishe hoja ambazo ndizo zinazosemekana au ndizo walizonazo zinazohusiana na suala nzima la hiyo sintofahamu, tuliyokuwa tunajaribu kuisema,” alisema Jaji Mutungi.
Jaji Mutungi alisema kikao cha Baraza la Vyama vya Siasa, kitafanyika tarehe 13 Oktoba 2021, visiwani Zanzibar.
Leave a comment