WANAWAKE nchini wameshauriwa kutumia teknolojia mbalimbali za kisayansi katika shughuli zao za kila siku ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Ushauri huo umetolewa leo tarehe 10 Machi, 2022 na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech), Dk. Philbert Luhunga wakati wa hitimisho la siku ya wanawake duniani lililofanywa na wanawake kutoka Costech jijini Dar es Salaam.
“Leo tupo hapa tunahitimisha Siku ya wanawake duniani, lakini tutakuwa na mdahalo unaohusisha wanawake kujua jinsi gani wanaweza kupambana na changamoto hii ya mabadiliko ya tabia nchi,” amesema.
Amesema, shughuli nyingi za wanawake zinahusisha mazingira na kutolea mfano kilimo na maji.
“Kwenye kilimo inabidi wajaribu kubadilisha mtindo wa zamani watumie pembejeo za kilimo na vile vile watumie teknolojia ya nishati mbadala kupika na kuachana na ile ya kizamani ya kukata kuni.
“Hapo zamani kuni na maji ni vitu vilivyokuwa vinapatikana kwa urahisi lakini nishati mbadala ya kupikia inahitajika hivyo teknolojia mbalimbali zinahitajika,” amesema.
Kwa upande wake Mtaalam wa masuala ya mazingira nchini kutoka E- Link, Shukuru Nyagawa amesema wanawake ndio wanaoathirika zaidi mabadiliko ya tabia nchi.
“Athari zinazompata mwanamke kukiwa na mvua, ukame, kimbunga, mabadiliko ya mabadiliko ya tabia nchi, kubwa ikilinganishwa na wanaume.
“Taarifa zinaeleza joto limeongezeka tumefikia kwenye nyuzi joto 1.1 inawezekana ikafikia nyuzi joto 1.5 ifikapo 2030. Ikifikia huko kutakuwa na athari kuwa kwenye uchumi wa jamii na wanawake ndio wanaoathirika zaidi,” amesema.
Aidha, naye Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ( UDSM), Dk. Magreth Samiji amesema wamebuni Mradi wa majiko ya sola ikiwa ni njia ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Amesema wamefanya utafiti huo wa majiko baada ya kwenda wilaya ya Isimani Iringa na kukuta wanawake wanapikia masalia ya mahindi pamoja na vinyesi vya wanyama.
Awali Dk. Harun Makandi mratibu wa utafiti kutoka Costech amesema tume hiyo imekuwa ni mshauri mkuu wa serikali na wadau wengine katika mambo yanayohusu utafiti na ubunifu.
Amesema Costech imekuwa ikisaidia kuandaa sera kuhusiana na maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na kuishawishi serikali ili kuitekeleza.
Leave a comment