SERIKALI imesema haitafunga mipaka kuwazuia wakulima na wafanyabiashara wanaotaka kuuza mahindi yao nje ya nchi. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yameelezwa na jana tarehe 22 Disemba, 2021 na Naibu wa Kilimo, Hussein Bashe alipofanya ziara ya kukagua ujenzi wa kiwanda cha mbolea kinachojengwa na wawekezaji kutoka Burundi katika eneo la Nala jijini Dodoma.
Bashe amesema kwa sasa Tanzania ina akiba ya chakula cha kutosha hivyo wafanyabiashara wanaouza chakula nje hawatazuiwa kuuza chakula nje ya nchi wala kupangiwa bei ya kuuza.
Pia Bashe amewataka wataalamu wa utafiti wa kilimo (TARI) pamoja na wataalamu wa Wakala wa Taifa wa hifadhi ya Chakula (NFRA) kukaa pamoja na wawekezaji wa kiwanda cha mbolea cha Itracom Fertilizers LTD ili kuweka mpangokazi wa kufanikisha mahitaji sahihi katika matumizi ya mbolea katika kila mkoa na wilaya zake.
Bashe amesema kwa kuwa kiwanda hicho kinategemea kukamilika mwezi wa saba mwaka 2022, mipango mikakati hiyo inatakiwa iwe imekamilika mwezi wa tano mwaka 2022 ili kupunguza changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza katika viwanda vingine vyauzalishaji mbolea.
“Tumeona changamoto ya matumizi ya mbolea katika maeneo mbalimbali, natoa maagizo kwa taasisi ya utafiti wa kilimo na wakala wa taifa wa hifadhi ya chakula kukaa pamoja na wawekezaji kutoka Burundi ili kuweka mpango kazi wa kubaini jambo la kufanya katika ufafiti wa mbolea ili kujua ni aina gani ya mbolea inatakiwa na ni sehemu gani.
“Naagiza vikao vyenu vifanyike na ifikapo mwezi wa tano muwe mmepata ufumbuzi kwani changamoto ambazo zimekuwa zikipatikana katika viwanda vingine vya kuzalisha mbolea zisije zikajitokeza katika kiwanda hiki,” amesema Bashe.
Katika hatua nyingine Bashe amesema asilimia kubwa ya mbolea itayotengenezwa na kiwanda hicho inatokana na samadi na ni lazima samadi zitakazopelekwa kiwandani kutengeneza mbolea zifanywe na wazawa.
Hata hivyo, Bashe amesema kwa kuwa wakulima wengi walitumia mbolea ya chumvichumvi imesababisha ardhi kupoteza ubora lakini kiwanda hicho kitazalisha chokaa kwa ajili ya kuhuisha ubora wa rutuba ya ardhi.
Kwa upande wa mwekezaji kutoka Burundi katika kiwanda hicho cha mbolea, Mhandisi Musafiri Dieudonne amesema ujenzi wa kiwanda hicho ni mkombozi mkubwa kwa mkulima wa Tanzania na watatoka katika kilimo cha kujikimu na kuwa kilimo cha biashara.
Amesema mpaka kiwanda kinakamilika kitakuwa kimegharimu dola za Marekani milioni 180 na kinatarajiwa kukamilika mwezi wa saba mwaka Jana.
Hata hivyo, amesema pamoja na ujenzi wa kiwanda hicho wanakabiliwa na changamoto ya uhaba wa maji na kukatika katika kwa umeme.
Leave a comment