WANANCHI wametakiwa kutoa ushirikiano katika madawati ya kijinsia ya Jeshi la Polisi, utakaowezesha kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumanne, tarehe 10 Mei 2022 na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Faidha Yusuph Suleimani, katika mafunzo ya elimu ya afya ya uzazi na masuala ya ukatili wa kijinsia, yaliyofanyika jijini Dodoma.
Kamanda Faidha ameitaka jamii kutoa taarifa za vitendo vya ukatili wa kijinsia katika madawati hayo, ili zifanyiwe kazi na wahusika wachukuliwe hatua za kisheria.
“Dawati la jinsia linafanya kazi kwa saa 24 kwa kuzingatia sheria na miongozi mbalimbali, ikiwemo maafisa ustawi wa jamii. Kumhudumia mhanga katika sura ya usiri ili kuhakikisha tunalinda haki na utu wa mhanga. Sisi wote tuna jukumu la kuelimisha jamii kupitia njia mbalimbali ikiwemo kutoa elimu katika shule zetu,” amesema Kamanda Faidha.
Katika hatua nyingine, Kamanda Faidha amewataka waandishi wa habari kuripoti habari za ukatili wa kijinsia kwa kufuata maadili na miiko ya taaluma yao, hasa habari zinazohusu watoto.
“Usitoe taarifa za kushutumiana, tunatakiwa tufanye shughuli zetu vizuri na kuhakikisha tunawalinda watoto dhidi ya ukatili na matukio mengine ya ukatili wa kijinsia katika jamii yetu,”amesema Kamanda Faidha.
Naye Meneja Mawasiliano wa Taasisi isiyo ya kiserikali ya Marie Stopes, Ester Shedafa, amesema shirika hilo lenye matawi takribani nchi nzima lianendelea kutoa huduma za afya ya uzazi kupitia program ya mikoba, kwa wananchi hususani wa pembezoni ya mji.
“Tunatoa huduma ya afya uzazi pamoja na utoaji wa mafunzo kwa vijana, juu ya namna ya kujitambua na kuweza kuripoti pale anapotendewa tukio la ukatili,” amesema Shedafa.
Leave a comment