WANANCHI wa kijiji cha Bulige kata ya Bulige katika halmashauri ya Msalala wilayani Kahama mkoani Shinyanga wamemkataa mwenyekiti wa kijiji hicho, mtendaji pamoja na wajumbe wa kamati ya maendeleo ya kata kwa upotevu wa mifuko 150 yenye thamani ya Sh. 1.5 milioni, anaadika Mwandishi Wetu.
Wakitoa kauli hiyo ya pamoja wakazi hao wa kijiji cha Bulige katika mkutano wa hadhara uliofanyika jana, wamesema kupotea kwa mifuko hiyo hawana imani na viongozi hao kwani pesa iliyotumika ni baada ya kuuzwa eneo ambalo ni mali ya kijiji kwa ajili ya kujenga chumba cha akina mama katika zahanati ya kijiji hicho cha Bulige.
Wakisisitiza wamesema kuwa mwenyekiti Matayo Jebu na Afisa mtendaji Ally Mapinda ndio watu muhimu katika kijiji, lakini kwa kitendo walichokifanya hakina manufaa ndani ya kijiji kwa kutoa thamani ya eneo isiyo sahihi kwa ajili ya manufaa yao binafsi hivyo wajiondoe wenyewe.
Mmoja wa wakazi hao, Kasule Lufunga alisema katika uuzwaji wa eneo hilo mkutano wa awali ulioitishwa na viongozi hao wananchi walipewa taarifa kuwa mnunuzi amepatikana kwa thamani ya Sh. 3.5 milioni.
Kwa upande wake mwenyekiti wa kijiji hicho, Mathayo Jebu alikiri kuwapo upotevu wa fedha hizo huku akisema wamekubali kuzirudisha, lakini kama wananchi wamefikia maamuzi hayo ya kutokuwa na imani nao hakuna haja ya malumbano wao wamelipokea.
Leave a comment