WAKATI watu zaidi ya milioni moja wakiripotiwa kuikimbia Ukraine, wengine wameamua kujitokeza na kuandamana barabarani kuzuia uvamizi wa majeshi ya Urusi. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamejiri wakati leo ikiwa ni siku ya nane tangu Urusi ianze kuivamia Ukraine na kulipua miji muhimu ya nchi hiyo iliyopo Barani Ulaya.
Aidha, katika video iliyoachiwa leo tarehe 3 Machi, 2022 na Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky kupitia mtandao wa Facebook, amewapongeza wananchi wake kwa kushikamana katika kuitetea nchi yao.
Huko kusini mwa jiji la Enerhodar wananchi wameandamana nje ya kituo cha kuzalisha umeme ikiwa ni jitihada za kuzuia jeshi la Urusi.
Kwingineko katika mji mkuu wa Ukreini, Kyiv wananchi wanafundishwa namna ya kutengeneza mabomu ya petrol ili kuyatumia kuzuia wanajeshi wa Urusi.
Jitihada hizo za wananchi zinaonekana kuzaa matunda kusini mwa jimbo la Zaporozhye ambapo video ya ndege isiyo na rubani (droni) imeonesha majeshi ya Urusi yakirudi nyuma.
Aidha, wakazi wa Melitopol kusini mwa Ukreini wamewagomea majeshi ya Urusi kuingia katika eneo hilo kwa saa mbili.
Inaelezwa kuwa msafara mkubwa wa magari ya jeshi la Urusi kuelekea katika mji mkuu Kyiv yamesimama kwa takribani saa 24 hadi 36 kwa kile kinachodaiwa ni kuishiwa mafuta pamoja na chakula, kwa mujibu wa ofisa wa usalama wa Marekani.
Leave a comment