MTANDAO wa Kupinga Ukatili wa Kijinsia (MKUKI) umelaani kitendo cha wanawake wanne wanaotuhumiwa kwa kosa la ukahaba, kudhalilishwa mitandaoni. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Picha za wanawake hao akiwemo Shania Hamada, Najia Alfani, Amina Mawazo zinazoonesha wakibeba mabango yenye makosa yao na mahali walipotenda, zilianza kusambaa katika mitandao ya kijamii, tangu jana tarehe 25 Julai 2019.
Wakili Anna Henga, Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) akisoma tamko la MKUKI leo tarehe 26 Julai 2019, amesema mtandao huo pamoja na wanaharakati wengine wanapinga kitendo hicho, kwa kuwa ni ukiukwaji wa haki za binadamu.
Wakili Henga ameeleza kuwa, kitendo hicho ni udhalilishaji wa utu wa mwanamke pamoja na kuingilia uhuru wao wa faragha.
Amesema picha hizo zilipigwa na maofisa wa polisi katika Kituo cha Polisi cha Murahati, na kwamba walizungumza na mkuu wa kituo hicho ambaye alithibitisha zilipigwa kituoni hapo kwa manufaa ya kazi, na si kusambazwa kama ilivyotokea.
Kufuatia hatua hiyo, MKUKI ameliomba Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua za kinidhamu waliohusika kusambaza picha za wanawake hao.
Leave a comment