MAMIA ya wanafunzi wamelivamia Bunge la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wakishinikiza walimu wao waongezewe mshahara. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Wanafunzi hao walikuwa wanapeperusha matawi na kuimba “tunataka kusoma, ikiwa hatutasoma, tutatumia dawa za kulevya”.
Kwa mujibu wa radio inayomilikiwa na Umoja Mataifa- Radio Okapi maandamano ya aina hiyohiyo yalitokea katika mji wa Beni kaskazini mwa Kivu.
Walimu wamekuwa katika mgomo tangu Oktoba 4, mwanzoni mwa masomo mwaka huu wakitaka waongezewe mshahara na kupunguza umri wa kustaafu pamoja na masuala mengine.
Serikali imewashutumu viongozi wa dini ambao wanasimamia shule nyingi za msingi, kwa kudai kuwa wanahusika na mgomo huo ingawa viongozi hao wamekanusha madai dhidi yao.
Makamu wa rais wa DRC, Jean-Marc Kabunda, amewataka wanafunzi kurudi nyumbani maana haya sio mapambano yao.
“Nyinyi sio watu wa mtaani, mnapaswa kuwa shuleni na kama hampo shule mnapaswa kuwa nyumbani,” alisema.
Aidha, Waziri wa elimu ya msingi nchini humo, Tony Mwaba amesema serikali imerejesha majadiliano kuhusu madai ya walimu hao ili kurejesha hali ya utulivu.
Leave a comment