SHULE tatu za msingi katika jimbo la New York nchini Marekani zimepiga marufuku mavazi ya ‘Halloween’ yanayofanana na yale yaliyovaliwa na washiriki wa tamthilia maarufu ya Netflix, Squid Game, kwa kuhofia kwamba yanaweza kuchochea vurugu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Tamthilia hiyo ya kusisimua ya Korea Kusini inaeleza kuhusu hadithi ya watu wazima wanaoshindania zawadi ya pesa kwa kucheza michezo ya watoto, na ambao wako tayari kuhatarisha maisha yao ili kushinda.
Maudhui yake yanayoonekana kwenda kinyume na maadili kwa baadhi ya jamii yamesababisha shule kuwatumia barua pepe wazazi kuhusu ujumbe wa uchochezi uliomo kwenye tamthilia hiyo.
Shule hizo zimesema mavazi ya mchezo wa Squid katika hafla za shule hayatafaa.
Mkuu wa Shule ya Fayetteville ya New York, Dk. Craig Tice amesema muongozo wa shule hiyo umepiga marufuku mavazi ya Halloween yenye vitu vinavyoweza kufasiriwa kama silaha na vya kutisha.
Nchini Marekani, tamthilia hiyo imewekwa na mtandao wa Netflix kwenye darala la kuangaliwa na hadhira ya watu wazima hii ikimaanisha kwamba tammthili hiyo haitakiwi kutazamwa na watoto chini ya umri wa miaka 17.
Aidha, baadhi ya wazazi wanaripotiwa kutofurahishwa na marufuku hiyo ya mavazi iliyotolewa na shule hizo.
“Ni vazi tu. Jambo la msingi ni kutoruhusu watoto wako kutazama tamthilia hiyo,” amesema mwanamke mmoja.
Leave a comment