BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetoa muda wa wiki mbili kwa wanafunzi ambao hawajakamilisha maombi ya mkopo kufanya hivyo kuanzia leo tarehe 1 Septemba, hadi 15, 2021. Anaripoti Noela Shila na Patricia Kighono, TUDARCo … (endelea).
Bodi imetoa maagizo hayo tarehe 1 septemba 2021 wakati ikizungumza na vyombo vya habari kuhusiana na mwenendo wa utoaji mikopo kwa wanafunzi elimu ya juu.
Mkurugenzi mtendaji wa HESLB, Abdul –Razaq Badru alisema mpaka sasa wamepokea maombi ya wanafunzi 91,445 ambapo asilimia 56 ya maombi hayo ni ya wanafunzi wa kiume huku asilimia 43 zikiwa za wanafunzi wa kike.
Badru alisema asilimia 86 ya maombi hayo yamekamilika wakati asilimia 13 yakiwa na makosa.
“Hivyo bodi imetoa wiki mbili kwa wanafunzi ambao hawajakamilisha maombi yao kukamilisha kwa kusahihisha makosa mbalimbali waliyofanya wakati wakiomba mkopo hapo awali.
“Baadhi ya makosa yaliyoainishwa ni pamoja na fomu kutosainiwa na muombaji, kutoambatanisha picha ya muombaji na mdhamini katika fomu ya maombi, kutokuambatanisha kitambulisho cha mdhamini katika fomu, fomu kutosainiwa na watendaji wa kijiji, fomu kutosainiwa na mwanasheria.
“Pia baadhi ya waombaji kutokuhakiki vyeti vyao vya kuzaliwa pamoja vyeti vya vifo vya wazazi,” amesema.
Aidha, amesema kwa wanafunzi waliopo katika mafunzo ya JKT ambao hawakupata fursa ya kuomba mkopo, bodi imewapa siku kumi za kufanya maombi hayo kuanzia tarehe 20 Septemba 2021 hadi 30 Septemba 2021.
Pia Shirika la Posta pamoja na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) wamesema wataendelea kushirikiana na bodi ya mikopo ili kuhakikisha wanafunzi wote ambao hawajakamilisha taratibu za kuomba mkopo wanafanya hivyo kwa haraka zaidi.
Vizuri sana kwani taarifa imeeleweka vizuri