WANAFUNZI 2,615 wa Shule ya Msingi Kanindo iliyopo Kata ya Kishili jijini Mwanza wanalazimika kusoma kwa zamu ili kuachiana vyumba vya madarasa vilivyopo kitendo ambacho kinaonekana kuwafanya walimu kushindwa kutimiza wajibu wao kikamilifu. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea)
Wingi wa wanafunzi hao ukilinganisha na vyumba sita vya madarasa vilivyopo, vimeufanya uongozi wa shule hiyo kuwagawa wanafunzi hao katika makundi mawili ambapo wanafunzi 1,302 ambao ni darasa la pili, la nne na sita wamewekwa kundi la kwanza.
Kundi la pili lina jumla ya wanafunzi 1,313 ambao ni darasa la awali, la kwanza, tatu, la tano na la saba huku ikikadiriwa kila darasa moja hulazimika kuingia wanafunzi zaidi ya 200 katika chumba kimoja na wengine kukaa chini kitendo kinachompa mwalimu ugumu wa kufundisha na kutambua uelewa wa watoto hao.
Akizungumza katika kikao cha kamati ya shule kilichowakutanisha wazazi na uongozi wa Serikali ya mtaa wa Kanindo, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Joseph Mhuli amesema mazingira yaliyopo hapo shuleni si rafiki kwa walimu na wanafunzi, hivyo kuna haja ya kuchukua hatua za dharula kujenga vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo.
Mhuli amewaomba wazazi pamoja na uongozi wa mtaa kwamba wanafunzi wanapata shida wanapokuwa darasa kwani darasa moja linachukua idadi kubwa ya watoto ambao wengine hulazikika kukaa chini wakati mwalimi akifundisha.
“Mtu mgeni akipita hapa shuleni atadhani wanafunzi wapo mapumziko kumbe sivyo, tunalazimika kuwatoa nje ili wengine waingie darasani ndio maana kila wakati watoto hawakosi nje, jambo lingine hivi vyumba vilivyopo ni vidogo sana vilijengwa kienyeji sana.
“Mfano darasa la tano lina wanafunzi 217 hawa wote wanaingia pamoja darasani, hebu fikiria wanakaaje humo, kwanza hewa haitoshi pia dawati moja wanakaa wanne na wengine wanalazimika kukaa chini karibu na ubao, mwalimu akifundisha anapita juu ya miguu ya wanafunzi.
“Pale matundu ya vyoo yaliyopo ni sita hayatoshi kwa idadi hiyo ya wanafunzi, ndio maana mnaona baadhi ya wanafunzi wanajisaidia nje na wengine mlimani, naombeni uongozi mtaa muone muhimu wa kujenga hata madarasa mawili au matatu, tunashukuru kamati ya shule imejitolea kujenga ofisi ya walimu kwa fedha zao na tunasubiri Serikali kuezeka,”alisema.
Kutokana na hali, Mtendaji wa Mtaa wa Kanindo, Petro Mashili na Mwenyekiti wa mtaa huo, Ndalahwa Masibuka aliwataka wananchi kuchangia nguvu yao ili kuanzisha ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa haraka.
Katika mkutano huo, wananchi waliazimia kila kaya kuchangia Sh 3,000 au kutoa matofali matatu ambayo yanapaswa kuwasilishwa shuleni ambapo mwisho ni Februari 30, mwaka huu ili ujenzi uanze Machi.
Wakati huo huo, mdau wa sekta ya elimu na mkazi wa Kanindo, Mussa Maziku aliamua kujitolea mwenyewe na kuahidi kujenga darasa moja ambapo tayari amewasilisha matofali 300 shuleni hapo.
Uamuzi huo aliuchukua baada ya kushuhudia mazingira halisi ya wanafunzi hao wanavyosoma kwa taabu na kushikwa uchungu ambapo amesema atalijenga darasa hilo haraka kwa kushirikiana na marafiki wake.kutokana na hadi hiyo Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mtaa wa Kanindo, Hamis Gulam alisema wanachama wa chama hicho watamuunga mkono Maziku kuhakikisha darasa hilo linakamilika haraka.
Leave a comment