RAIS wa Jamhuri, Samia Suluhu Hassan, amemteuwa Camillus Mongoso Wambura, kuwa mkuu mpya wa jeshi la polisi nchini (IGP). Anachukua nafasi ya Simion Sirro, ambaye amefanywa kuwa Balozi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais (Ikulu), Sirro amefanywa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe. Sirro alitarajiwa kustaafu jeshi la polisi mwaka huu.
Kabla ya uteuzi huo, Wambura ambaye amewahi kushika nyadhifa mbalimbali, ikiwamo Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kanda Maalum ya Dar es Salaam (ZCO), alikuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya jinai nchini (DCI).
Naye aliyekuwa Kamishena Msaidizi wa Polisi (ACP) na Kamanda wa Polisi mkoani Kigoma (RPC), Ramadhani Kingai, amepandishwa cheo na kufanywa kuwa DCI.
Hata hivyo, muda mfupi baada ya tangazo hilo la uteuzi, mijadala imeibuka kwenye mitandao ya kijamii, hasa kuhusiana na uteuzi wa Kingai.
Baadhi ya wananchi waliotoa maoni yao, wanakosoa uteuzi wa Kingai, kama mtu asiyestahili kushika wadhifa huo, kwa madai kuwa ni miongoni mwa maofisa wa Polisi, walioharibu taswira la jeshi hilo.
Wanasema, Kingai ametajwa katika matukio mbalimbali ya ukiukwaji wa haki za binadamu, ikiwamo kubambikizia raia kesi.
Kama Rais Samia angetaka kujijenga kisiasa, basi Kingai hakupaswa kuingia kwenye uteuzi huu, hasa kwa kushika wadhifa mkubwa kama huu,” ameandika mmoja wa wachangiaji kwenye mtandao mmoja wa kijamii.
Aidha, Rais amemteuwa Dk. Suleiman Haji Suleiman, ambaye alikuwa afisa katika wizara ya Mambo ya Nje na Ushiriako wa Afrika Mashariki, kuwa Balozi.
Wengine walioteuliwa, ni Kamishena wa Polisi (CP), Liberati Sabas Materu, kuwa Kamishena wa Fedha na Logistiki. Anachukua nafasi ya Hamad Khamis Hamad.
Leave a comment