SERIKALI imesema kuwa kila mwananchi aliyeomba kiwanja kwa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) kuwa kiwanja chake hakitapotea baada ya mamlaka hiyo kuvunjwa, anaandika Dany Tibason.
Kauli hiyo ilitolewa leo bungeni na Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu alipokuwa akijibu swali la Matha Mlata, Mbunge wa Viti Maalum (CCM).
Katika swali lake, Matha alitaka kujua nini hatma ya wananchi walionunua viwanja na hawajakabidhiwa na CDA na kwa sasa imevunjwa.
Waziri Mjaliwa amesema kwa sasa shughuli zote za CDA zimehamishiwa kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma na akaunti zake zote zimefungwa na ukaguzi wa kina unaendelea kujua kuna kiasi gani na matumizi yake.
Amesema mara baada ya kukamilika kwa ukaguzi huo shughuli zitarejea kama kawaida lakini zitafanywa na halmashauri ya Manispaa ya Dodoma na huduma katika jengo lilokuwa la CDA zitaendelea na hapo hapo kutakuwa na Idara ya Ardhi.
“Tunataka mtu akiingia katika jengo hilo anaomba kiwanja na wakati huo huo anapata hati yake na jengo lile tunataka liandikwe ‘CDA idara ya ardhi’,’’ amesema.
Amesema kutokana na baadhi ya watumishi walikuwa wakilalamikiwa sana na wananchi hivyo watumishi hao watawekwa kando kabla ya kuhamishiwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma na kuzitaka halmashauri zote nchini kuzingatia sheria pale wanapotwaa maeneo ya wananchi kwa kulipa fidia.
Aidha amesema ni lazima fidia ilipwe kwanza kabla ya kutwaa maeneo hayo na ilingane na thamani ya eneo husika.
‘’Zipo Sheria zonzoongoza katika masuala ya fidia na maeneo yote ni lazima yalipie fidia kwanza kabla ya kuyatwaa kwani wengine wanaweza kuwa na mazao katika maeneo hayo’’ amesema.
Leave a comment