HALFAN Bwire Hassan, mlinzi wa Mwenyekiti wa Chama cha Chadema, Freeman Mbowe, amesomewa shtaka la kumiliki sare na jeshi kinyume cha sheria. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Hassan amesomewa shtaka hilo kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, leo Ijumaa, tarehe 6 Agosti 2021 na Wakili wa Serikali Pius Hilla, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa mahakama hiyo, Thomas Simba.
Akisoma shtaka hilo, Hilla alidai kwamba, Hassan alitenda kosa hilo tarehe 10 Agosti 2020, Temeke mkoani Dar es Salaam, ambapo alimiliki sare hizo kinyume cha sheria kwa madhumuni ambayo ni hatari kwa usalama wa Taifa.
Hilla alidai, Hassan alikutwa na pea nne za sare, kofia tano, overoll moja, soksi pea nne na sweta moja ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Pia, anadaiwa kukutwa na suruali moja ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), na kisu kimoja.
Mlinzi mwingine wa Mbowe, Adam Hassan Kasekwa, alisomewa shtaka la kukutwa na silaha aina ya Pisto, bila kibali kinyume cha sheria, anadaiwa kutenda kosa hilo tarehe 5 Agosti 2020, wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro.
Kwa mujibu wa Hilla, Kasekwa anatuhumiwa pia katika shtala la kukutwa na risasi tatu isivyo halali na kinyume cha sheria, akidai kwamba mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo tarehe 5 Agosti mwaka 2020, wilayani Moshi Mkoa wa Kilimanjaro.
Baada ya Hilaa kuwasomewa mashtaja hayo walinzi wa Mbowe, Hakimu Simba aliwataja wasiyajibu kwa maelezo kwamba mahakama hiyo haina mamlaka ya kuyasikiliza.
Washtakiwa hao walipomaliza kusomea mashtaka, Hakimu Simba aliahirisha kesi hiyo hadi tarehe 13 Agosti 2021.
Hakimu Simba aliahirisha kesi hiyo baada ya upande wa Jamhuri kudai Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), kutokamilisha taratibu za kuipeleka kesi ya ugaidi inayowakabili walinzi hao na Mbowe, katika mahakama yenye mamlaka ya kusikiliza.
Halfan na Adam ni miongoni mwa washtakiwa wanne akiwemo Freeman Mbowe na Mohammed Abdillah Lingwenya wanaotuhumiwa kwa mashtaka sita yakiwemo ya kupanga njama za ugaidi pamoja na uhujumu uchumi.
Leave a comment