JESHI la Wananchi Tanzania (JWTZ) limesema hakuna walinda amani Watanzania wanaoshikiliwa wala kuhusika na mauji ya raia nchini DRC. Anaripoti Jonas Mushi, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza kwa njia ya simu na MwanaHALISI Online, Msemaji wa JWTZ, Luteni KanalI, Gaudentius Ilonda, alipoulizwa kuhusu taarifa hizo amesema “hakuna kitu kama hicho.”
Ameongeza kuwa walinda amani Watanzania waliopo DRC wanaendelea kutekeleza majukumu yao ya kulinda amani kwa mujibu wa Sheria, taratibu na kanuni za Umoja wa mataifa.
“Hakuna mwanajeshi Watanzania aliyekamatwa na hakuna mwanajeshi Watanzania aliyefanya hivyo ulivyosikia kama umeona BBC waulize waliokamatwa ni Watanzania ipi.
“Wanajeshi wetu waliopo kule wapo kwenye ulinzi wa amani na wanaendelea na ulinzi wa amani kwa mujibu wa Sheria na taratibu na kwa kanuni za Umoja wa Mataifa hakuna ambaye amekamatwa au amefanya nini, hakuna kitu kama hicho,” amesema Luteni Kanali Ilonda.
BBC imeripoti kuwa imezungumza Naibu Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa MONUSCO, Khassim Diagne, na kwamba amesema walinda amani waliokamatwa kwa tuhuma za mauji ya raia nchini DRC ni Watanzania.
Hata hivyo taarifa hiyo ya BBC haina uthibitisho wowote ikiwemo wa majina ya walinda amani hao ili kujua kama kweli ni Watanzania au la.
Wanajeshi wa Tanzania kwa muda mrefu wamekuwa msaada mkubwa katika vikosi vya walinda amani wa Umoja wa Mataifa katika kamisheni mbalimbali za umoja huo kwenye mataifa ambayo hayana amani ikiwemo DR Congo, Somalia, Lebanon, Sudani na zingine nyingi.
Tanzania imekuwa ikijizolea sifa Kimataifa katika kamisheni za kulinda amnai kutokana na uhodari na nidhamu ya wanajeshi wake.
Katika kipindi cha juma moja lililopita watu kadhaa wamefariki katika maandamano ya ghasia dhidi ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa wanaojulikana kama MONUSCO.
Waandamanaji hao walishambulia kambi mbili za Umoja wa Mataifa huko Goma na Butembo, ambapo walinda amani wanne wa Umoja wa Mataifa waliuawa.
Walinda amani wawili kati ya hao walikuwa raia wa Morocco na wengine wawili walikuwa Wahindi, wote walikuwa wamefanya kazi nchini DR Congo kwa Umoja wa Mataifa kwa muda wa chini ya miezi sita – huku mmoja wa waliouawa akiwa amekaa kwa miezi miwili na siku 22 pekee.
Mwezi Juni vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa viliondoka katika jimbo tofauti la mashariki – Tanganyika – baada ya kile walichokieleza kuwa kuimarika kwa hali ya usalama.
Leave a comment