WATAFITI wa mbegu waliopo kwenye vituo 16 vya Utafiti wa mazao mbalimbali hapa nchini wameshauriwa kuhakikisha mbegu wanazozalisha kwanza zinatumiwa na wakulima wanaozunguka vituo vyao na baadae wazifikishe kwa wakulima wengine wa mbali. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa kilimo Tanzania (TARI) Dk. Geofrey Mkamilo amesema hayo jana kwenye uzinduzi wa ofisi ya TARI iliyopo kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere vya maonesho ya wakulima 88 kanda ya mashariki na kwamba matumizi hayo ya mbegu kwa wakulima wa jirani na vituo yatasaidia wakulima wengine kuona umuhimu wa vituo hivyo.
Amesema kuwa watafiti mbalimbali kupitia vituo hivyo wamekuwa wakitengeneza mbegu mbalimbali zikiwemo za mazao ya chakula na biashara lakini wamekuwa wakifikisha elimu hiyo kwa wakulima waliopo mbali na vituo na kuwaacha wakulima wa maeneo yao jambo ambalo wakati mwingine halileti maana.
“Haiwezekani kukawa na kituo cha utafiti katika eneo halafu wakulima wa eneo husika hawanufaiki na wanaendelea kulima kwa kutumia mbegu za zamani bila kutumia teknolojia nzuri zilizopo,” amesema.
Pia Dk. Mkamilo amesema kuwa kuhimiza matumizi ya mbegu bora kwa wakulima waliopo jirani na vituo vya utafiti itasaidia hata wakulima wengine kutoka maeneo ya mbali kuweza kupata elimu na kujifunza kabla ya kuanza kutumia mbegu na teknolojia za utafiti zinazozalishwa na vituo hivyo.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Injinia Matwew Mtigumwe amewataka wakulima kuzitumia mbegu na teknolojia zinazotolewa na watafiti ili kuweza kuinua sekta ya kilimo na kufikia malengo yanayokusudiwaa.
Injinia Mtigumwe amesema kuwa matumizi ya mbegu zilizopitishwa na watafiti yanaweza kuinua uchumi wa jamii kupitia kilimona pia kufikisha nchi katika suala zima la Uchumi wa Viwanda.
Leave a comment