JUKWAA la Wakulima wanawake wilayani Chamwino (JUWWACHA) limeishauri serikali kutilia mkazo matumizi ya mbegu za muda mfupi ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi wilayani humo. Anaripoti Dany Tibason, Dodoma … (endelea).
Akisoma mapendekezo ya jukwaa hilo linalowezeshwa na Shirika la Action Aid, Mhasibu wa jukwaa hilo, Nuru Mpanda alisema kutokana na wilaya hiyo kukabiliwa na changamoto mbalimbali kwenye msimu wa kilimo wanashauri mkazo huo utiliwe ili waweze kupata mavuno mengi.
Pamoja na hayo, alisema pia serikali ipanue na kuimarisha mifumo ya umwagiliaji kama ilivyo kwa kata za Buigiri, Chalinze, Fufu, Suli na Chiboli ili kukabiliana na hali hiyo.
“Pia tunapendekeza mashine ya kupima afya ya udongo zinunuliwe na zitumike vijijini kwa ajili ya kuimarisha matumizi sahihi ya mbolea na mbegu,” alisema.
Alieleza kuwa wananchi wengi hawatumii mbolea kwa sababu mbalimbali, ikiwemo matumizi yanayohitaji kujua afya ya udongo ili kujua upungufu wa madini yanayokosekana kwenye udongo.
Alisema uwepo wa mashine hizo na huduma bora za ugani zitasaidia uzalishaji wa mazao wenye tija kwa wakulima.
Aidha alitaka taarifa za hali ya hewa kwa wakulima zitolewe kwa wakati ili wakulima waweze kujua kiwango cha mvua kilichopo kwenye maeneo yao.
Kadhalika, alisema changamoto nyingine zinazowakabili wakulima ni bei ya pembejeo kuwa ghali na kusababisha mkulima mdogo kushindwa kumudu.
Alisema kwa zao la alizeti mbegu ni ghali ambapo zinauzwa kuanzia Sh. 8,000 hadi Sh. 35,000 kwa kilo moja kutegemea na aina ya mbegu.
Awali, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, Samweli Kaweya aliwataka wakulima hao kutumia maghala ya ushirikia ili kuepuka janga la kuuza mazao bila sababu za msingi.
Alisema wakulima wengi wamekuwa wakiuza mazao bila utaratibu wa kutohifadhi mazao katika maghala ya kuhifadhia mazao hayo na kusababisha familia nyingi kukosa chakula.
Leave a comment