JUMLA ya vikundi 46 vya wakulima wa mazao mbalimbali mkoani Morogoro wameanza kuondokana na adha ya kukosa masoko ya bidhaa zao kufuatia kukutanishwa na wanunuzi na viwanda vya kusindika bidhaa. Anaripoti Christina Haule … (endelea).
Akizungumza na wakulima hao, Meneja wa vikundi vya uhamasisha kilimo mkoa Morogoro, Ester Upendo Kasai amesema kuwa ameamua kuwakutanisha ili kuboresha upatikanaji wa masoko kwa wakulima na kuinua kilimo ndani ya mkoa wa Morogoro ambao ndiyo mkoa wa kwanza kuzalisha mazao mengi lakini hukosa masoko.
Kasai amesema kuwa kufuatia wakulima hao kupata masoko wanaweza kuweka benki ya chakula kitakachoweza kusaidia kulisha na kufanya biashara za ndani na nje na hivyo kukuza uchumi wa mkulima na Taifa kwa ujumla.
Wakulima hao akiwemo John Mwamaso walikishukuru kikundi cha Uhamasishaji kwa kuweza kuwakutanisha na kupata masoko ya uhakika ambayo yataweza kuwasadia kuuza bidhaa zao na hatimaye kuwa na msimamo wa biashara za kilimo.
Aidha Mwamaso amesema kuwa kukutanishwa huko pia kutawasaidia kuweza kukopesheka tofauti na zamani kwamba mkulima hakopesheki kufuatia kuwakutanisha na Benki ya NMB ambako tayari wameshafungua akaunti zao kwa ajili ya kuendeleza kilimo.
Mmoja wa wanunuzi wa bidhaa hizo ambao ni Meneja wa Kampuni ya uzalishaji mazao ya Kilimo Tanzania, (Mahashree Agro-Proccesing Tanzania Limited), Benward Ndunguru amesema wameamua kuanza ujenzi wa kampuni ya kusindika mazao katika eneo la Mikese mkoani hapa ujenzi ambao utakamilika mwanzoni mwa mwaka ujao ili kununua bidhaa za kilimo na kuzisindika, kuongeza thamani na kuziuza katika nchi mbalimbali duniani.
Aidha amesema kuwa kufuatia kuanzishwa kwa kampuni hiyo wameshaanza kupokea bidhaa za kilimo kutoka kwa wakulima ikiwa ni pamoja na Korosho, Mbaazi, Ufuta, Karanga, Choroko na Dengu ambapo aliwaasa wakulima kuchangamkia fursa hiyo kwa kupeleka mazao yenye ubora.
Ndunguru amesema kuwa baada ya kuanzishwa kwa kampuni hiyo wataingia mkataba na vikundi vya wakulima ili waweze kupata mazao kwa wakati na wakulima kunuika kwa kuuza bidhaa zao na kulipwa kwa wakati.
Naye Meneja Meneja Mahusiano Kilimo biashara Kanda ya Mashariki kutoka benki ya NMB Christian Kihwelo aliwashauri wanavikundi hao kuhakikisha vikundi vyao vinasajiliwa au kupitishwa ili waweze kupata mikopo ya kuendeleza shughuli zao kufuatia wao kuwa wameanza kukopesha kwa wakulima wadogo tangu zamani kupitia Halmashauri, Brela au Rita na Ushirika.
Aidha Kihwelo amesema kuwa kufuatia wakulima hao kuingia mikataba ya biashara na wawekezaji pia wanaweza kupata nafasi ya kukopesheka kutokana na kuwa na uhakika wa masoko.
Hivyo aliwashauri kuzingatia mikataba watakayoingia na wawekezaji ili waweze kulipa mikopo watakayokopa kwa wakati na kufanya wengine kuendelea kukopa.
Leave a comment