WAKULIMA wa alizeti mkoani Singida, wamemwomba Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo, kuishauri serikali iongeze kodi ya mafuta ya kula yanayoingizwa nchini, ili kuinua uchumi wa wakulima, hususani wa wilaya ya Mkalama. Anaripoti Mwandishi Wetu, Singida … (endelea).
Akiwa kwenye ziara yake ya siku ya nne mkoani Singida, Chongolo alielezwa kuwa, baada ya uzalishaji wa zao hilo kuongezeka, kutokana na uhamasishaji mkubwa uliofanywa na serikali pamoja na wadau wake msimu wa 2021/22, hivi sasa bei imeshuka, kiasi cha kuathiri uchumi na hata pia kukatisha tamaa wenye nia ya kuendeleza zao hilo.
Wakizungumza kwenye mkutano wa tawi la CCM shina namba tano katika kijiji cha Iguguno wilaya ya Mkalama mkoani Singida, wakulima hao wamemweleza Chongolo, kuondolwa kodi mafuta ya kula kutoka nje, kumesababisha bei ya alizeti kushuka.
Akifafanua juu ya suala hilo, mbunge wa jimbo la Iramba Mashariki (Mkalama), Francis Isack, amesema kuwa, hivi sasa miongoni mwa wakulima wa alizeti wilayani humo kuna kiwango kikubwa cha alizeti, kutokana na bei kushuka, kutoka zaidi ya Sh. 100,000 kwa gunia la ujazo wa kati ya kilo 65 na 75, hadi kufikia chini ya Sh. 80,000.
Alisema kuwa, ikiwezekana anaiomba serikali iinunue alizeti hiyo ya wakulima iliyopo kwenye maghala mbalimnali, ili kuwapunguzia wakulima machungu ya uwepo kwa wingi wa alizeti wilayani humo.
Baada ya maelezo hayo, Francis alimwomba Katibu mkuu, awasilishe ombi lao serikalini, ili kunusuru uchumi wa wananchi wa Mkalama, ambao asilimia kubwa shughuli zao zinategemea zaidi kilimo, huku alizeti likiwa zao kuu la biashara.
Akijibu ombi la wananchi wa wilaya ya Mkalama, Katibu mkuu alikubali kupokea tatizo hilo na kuahidi kuondoka nalo kulipeleka kunakohusika, tayari kwa ajili ya kutafutiwa suluhu ya kudumu.
“Hii ni hoja ya msingi sana kwa sababu wananchi na wakulima wetu wamehamasika, wakaongeza uzalishaji wa alizeti…hili nimelichukua anaondoka nalo kulifikisha kwa wenzangu ili lifanyiwe kazi,” alisema Chongolo.
Leave a comment