MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam leo tarehe 12 Septemba 2019, imeombwa kulielekeza Jeshi la Magereza kuruhusu Mwandishi wa Habari za uchunguzi Erick Kabendera kupata matibabu, kutokana na afya yake kkuzidi kuzorota. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Mbele ya Hakimu Augustine Rwizile, Wakili wa Kabendera, Jebra Kambole amedai, hali ya mwanahabari huyo ni tete kiasi kwamba mguu wake wa kulia unashindwa kutembea kutokana na kupooza, pia kupata shida ya kupumua nyakati za usiku.
Pia, Wakili Kambole ameiomba mahakama hiyo kulielekeza Jeshi la Magereza kutoa taarifa rasmi ya ugonjwa unaomsumbua Kabendera.
Pia, Kabendera ameieleza mahakama hiyo kuwa anapata maumivu makali ya paja na mfupa wa mguu wa kulia, na kwamba alipimwa damu na kuchomwa sindano tatu zilizosaidia kupoteza tatizo kwa muda.
Kwa upande wake Wakili wa serikali Wankyo Simon, ameiambia Mahakama kuwa upelelezi wa kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili Kabendera bado haujakamilika katika baadhi ya maeneo.
Hata hivyo, Wakaili Simon hakuieleza mahakama hiyo maeneo gani ambayo upelelezi haujakamilika, baada yakuombwa na Wakili wa utetezi kufanya hivyo.
Baada ya maombi hayo, Hakimu Rwizile ameiharisha kesi hiyo hadi Septemba 18 mwaka huu itakapotajwa tena na kumtaka Kabendera kukutana na daktari wake siku ya kesho, kisha kuja kuieleza mahakama kinachoendelea kuhusu afya yake pale kesi yake itakapotajwa tena.
Kabendera anakabiliwa na mashtaka matatu ikiwemo madai ya kujihusisha na genge la uhalifu, kukwepa kodi kiasi cha Sh 173,247,047.02 na utakatishaji fedha, makosa ambayo hayana dhamana. Kabendera alikamatwa nyumbani kwake Mbweni tarehe 29 Julai mwaka huu.
Leave a comment