SERIKALI ya Tanzania na Bunge, imepewa muda wa siku 30 kuuvunja mkataba wa ushirikiano wa kiserikali kati yake na Imarati ya Dubai, kuhusu uwekezaji bandarini, pamoja na kuweka wazi mikataba mingine iliyoingiwa kuhusu uwekezaji huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 5 Septemba 2023 na Wakili Boniface Mwabukusi, akizungumza kwa niaba ya taasisi ya Sauti ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Mwanasiasa huyo aliyemstari wa mbele kupinga mkataba huo akidai hauna maslahi kwa taifa, ameitaka Serikali ndani ya siku 30, kuweka wazi kwa umma mikataba mingine kuhusu uwekezaji huo, ikiwemo kuchapisha magazetini na kwenye halmashauri ili wananchi waisome.
“Tatizo la mkataba huu haurekebishiki ni mkataba ambao hauna vigezo kabisa hata vya kurekebisha, kwa hili tunaomba waziri mwenye dhamana apeleke bungeni ili Bunge likafute azimio lake na hili lifanyike ndani ya siku 30. Ndani ya siku hizi tutaiandika rasmi serikali iweke wazi mikataba mingine yote waliyoingia ili tuone ina matatizo gani,” amesema Wakili Mwabukusi.
Wakili Mwabukusi amedai kuwa, kama Serikali haitatekeleza uamuzi huo, watachukua maamuzi magumu ikiwemo kuitisha maandamano ya amani, hadi mkataba huo utakaovunjwa.
“Baada ya siku 30 kama serikali haitafanya hivyo, tutakapoitisha maandamano tusilaumiwe na sio Mwabukusi atajificha nitakuwa mstari wa mbele kuongoza maandamano. Tuliwapa muda wanafanya utani tunawapa muda tena kama wasipofanya tutaingia barabarani na hatuaacha mpaka IGA iondoke. Kama IGA itakuwa milele tutaandamana milele kama itaondoka tutaacha,” amesema Wakili Mwabukusi.
Wakati Wakili Mwabukusi akidai mkataba huo una dosari, mara kwa mara Serikali imekuwa ikisisitiza kwmaba mkataba huo una maslahi kwa taifa, huku ikiahidi kufanyia kazi maoni ya wadau juu ya namna ya kurekebisha vifungu vyake vyenye mapungufu.
Leave a comment